NASAHA
Na. 047 Jumatano Mei 10 - 16, 2000
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
Ushauri Nasaha

Jukumu la wazazi, walimu kwa wanafunzi wanaomaliza masomo

NA KHADIJA IDD 

SI jambo geni kwa watu waliopitia shule za sekondari kuwa na matatizo, wasiwasi au hata kugombana wakati wanapokaribia kumaliza au wanapomaliza masomo yao. Ugomvi au matatizo haya yanatokana na kukosekana kwa msaada unaohitajika na unaofaa wakati mwanafunzi husika anapohitimu masomo yake; au kutokana na kulazimishwa na mzazi au mlezi kusoma masomo ambayo mwanafunzi huyo hayapendi. Ni wanafunzi wachache wanaopata wasaa wa kukaa na walimu au wazazi wao kujadili kwa mapana juu ya kile mwanafunzi huyo anachohitaji au kinachomfaa kuhusu maisha yake ya baadaye.
 

KATIKA kipindi hiki ambacho kidato cha sita wanafanya mitihani yao ya mwisho, wazazi au walezi wana jukumu kubwa sana la kuwasaidia watoto na wanafunzi wao. Kuwatakia wanafunzi mitihani myema na kuwahongera wanapomaliza mitihani na kufaulu haitoshi. Lakini waangalie kwanza wamewasaidia vipi kuelewa na kuchagua kozi na kazi watazochukua baada ya matokeo ya mitihani hiyo kutoka. 

Pamoja na kwamba muda mwingi wa watoto wao unapita wakiwa shule na wakati mwingine "tution", wazazi wana jukumu la kuzungumza na watoto wao na kuwashauri kwa wakati huo huo mdogo uliopo. Wanaweza kuwauliza maoni yao juu ya masomo yao na juu ya yale wanayoyapendelea na kujadili iwapo yanafaa kulingana na hali halisi ya maisha au la. Wazazi wanaweza kuchukua fursa hii kuchambua masomo au kozi zilizochaguliwa na watoto wao na kuangalia kazi wanazoweza kufanya kutokana na masomo hayo. 

Iwapo mzazi hana ujuzi juu ya masomo anayosoma mtoto wake au hajui kabisa juu ya mambo yanayohusu shule bado wana nafasi ya kumsaidia mtoto. Mzazi anaweza kuzungumza na walimu wa mtoto wake ili waweze kumsaidia kama wako karibu. Iwapo pia mtoto huyo anasoma shule ambayo iko mbali na nyumbani ya bweni, mzazi anaweza kukuwasiliana nao kwa simu au barua. Anaweza pia kumtafuta mtaalam wa masomo yake aliye karibu. Magazeti na majarida yanaweza kumsaidia kupata taarifa juu ya vyuo mbalimbali na mahitaji yake. Radio na Televisheni pia zitampa taarifa muhimu anazohitaji kupitia matangazo ya vyuo na kozi mbalimbali na namna ya kuwasiliana nao. Baada ya kupata taarifa hizi unaweza kuwasiliana na vyuo hivyo wewe mwenyewe na ukapata taarifa unazohitaji kufahamu kama vile masomo yanayofundishwa, muda, vyeti vinavyotolewa, mahal ichuo au shule ilipo n.k. 

Cha msingi hapa ni kushirikiana na mtoto wako ili aweze kupita vizuri katika kipindi hiki kigumu vile vile asipitie katika ugumu ambao wazazi na ndugu zake walipitia. Mzazi amsaidie mtoto wake afahamu baada ya masomo ya kidato cha nne atasoma nini, au baada ya kidato cha sita atasomea kozi gani na wapi na kwa muda gani. Hili litamfanya mtoto wako asome kwa malengo sio tu kwa vile alifaulu darasa la saba na amepitia sekondari. Lakini pia mzazi atasaidiana na walimu katika kuwasaidia wanafunzi husika, wakati mwingine pia mzazi atakuwa ana kumbusha mwalimu juu yasuala hili pale wanaposahau kufanya hivyo. 

Pamoja na jukumu hili la wazazi, walimu wana nafasi kubwa sana juu ya kumshauri mwanafunzi juu ya masomo yake ya baadaye. Ukubwa wa nafasi hii umetokana hasa na hali halisi kwamba, walimu wako pamoja na wanafunzi kwa muda mrefu na pia kwa sababu wanawafahamu wanafunzi wao na uwezo wao katika masomo wanayochukua. Pamoja na hayo, wana uwezo na ujuzi wa kutoa ushauri kama walimu na kama washauri na vile vile wanazo taarifa za kozishule navyuo mbalimbali vinavyowafaa wanafunzi wao. 

Kutokana na uwezo na nafasi zao, walimu wanaweza kuwasidia wanafunzi wao kwa kuwapatia taarifa juu ya kozi na vyuo mbalimbali hata kabla ya kuanza mwaka wao wa mwisho shuleni. Mwalimu anaweza kuwabandikia taarifa hizi katika mbao za matangazo au kuziwasilisha kwao ana kwa ana. 

Hata hivyo hili ni jambo ambalo walimu wote wanalifahamu na wanafahamu pia majukumu yanayowakabili katika suala hili. Ila ni walimu wachache sana ambao wanatekeleza hili. Ni wakati muafaka basi kwao kutekeleza ualimu wao hasa katika wakati huu ambao una matatizo ya ajira, utitiri wa vyuo na hali ngumu ya maisha. 

Walimu wana deni la kulipa, nalo ni hili la kuwasaidia wanafunzi wao kuelewa watakwenda wapi na watafanya nini mara watakapomaliza masomo yao. Vyuo viko vingi sana siku hizi ni jukumu la walimu kuwasaidia wanafunzi wao kuchagua wanavyovihitaji na vinavyowafaa. Vyombo vya habari vitumiwe na walimu kuwapatia wanafunzi taarifa zinazofaa. Walimu wawasaidie pia katika kuwatafutia wataalam kutoka sehemu mbalimbali ambao watawafahamisha wanafunzi juu ya taaluma zao, kama vile kutoka sekta ya utalii, kitivo cha sheria, vyuo vya ualimu, uhandisi, udaktari n.k. 

Mzazi na mwalimu aone jukumu la kumshauri mwanafunzi/mtoto wake ni lake. Kila mmoja achukue jukumu lake na amsaidie kijana husika tusingoje mpaka muda umekwisha, bali tumsaidie mapema ili awe na malengo na mwelekeo. 
 

Juu
 

YALIYOMO
 

TAHARIRI
Mazingira ya uchaguzi huru na haki yasivurugwe

Wananchi washutumu vyombo vya habari

Lipumba awaambia wananchi wasibabaishwe na walioko madarakani

Wasomi SUA walaani ‘rushwa’ ya kisiasa

Polisi kataeni kutumiwa - Lipumba 

Maelfu ya tani za matunda yanaoza Tanga

Habari za ndani
Uondoeni ‘ukoloni’ wa CCM- Mbukuzi

MPASHO NASAHA
WABONGO HAWANA NYONGO !

HABARI
Nchi wafadhili wataka upinzani,  CCM yalalama

Waislamu Musoma walalamika

Habari za Kimataifa

Ushauri Nasaha
Jukumu la wazazi, walimu kwa wanafunzi wanaomaliza masomo

Makala
Madhara ya ulevi kwa binadamu

MAKALA
Sababu ‘1000’ kwanini tunataka CCM ing’oke madarakani - 6

MAKALA
Kiini macho cha msamaha wa deni

Kalamu ya Mwandish
Kama CUF ni chama cha Waislamu 
Jee, CCM ni chama cha Wakristo?

MAKALA
Chama cha Mapinduzi na sera za maendeleo (2)

RIWAYA
Mapinduzi ya fikra

Lishe
Jinsi ya kuzuia utapiamlo kwa wanawake

BARUA

MASHAIRI

MICHEZO

  • Real Madrid yaingia fainali
  • Mapunda, Makoye hawafai timu ya Taifa - Kipingu
  • Tarimba ashinikizwa kujiuzulu Yanga

  •  

     


       Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com

    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita