NASAHA
Na. 043 Jumatano Aprili 12- 18, 2000
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
MICHEZO
 
 

Madadi, Jamhuri acheni 'rusha roho' katika soka ­ Wapenzi 

Na Mwandishi Wetu

WAPENZI wa soka wa mkoa wa Dar es Salaam wamewataka makocha Salum Madadi na Jamhuri Kihwelo wa timu za Kariakoo United na Kajumulo World Soccer kuacha malumbano nje ya uwanja na badala yake waoneshe ubora wao viwanjani kupitia timu zao.

Wito huo umekuja kufuatia malumbano baina ya makocha hao yaliyojikita ndani ya majigambo, kejeli na dharau dhidi ya mwingine katika medani ya soka. 

Hivi karibuni Madadi aliiponda timu ya Kihwelo kuwa ni mbovu na inayocheza bila malengo wakati Kihwelo alidai kuwa timu ya Madadi haina cha kujivunia zaidi ya kutegemea uzalendo mkoani Lindi. 

Wamewataka Madadi aliyewahi kuwa kocha wa Simba na Jamhuri aliyekuwa mchezaji wa timu hiyo kuachana na mipasho na badala yake wafundishe mpira. 

Jumamosi iliyopita timu timu ya Kajumulo ililazimisha sare ya bao 1-1 dhidi ya Kariakoo United katika mchezo wa ligi kuu Tanzania Bara uliofanyika mkoani Lindi. 


Kufuatia ushindi wa Juma Salum Simba:
Yanga wakumbwa na kiwewe 
  • Tarimba apatwa na kigugumizi, ataka Kahigi azungumzie 


Na Hamis Kasabe 

WANACHAMA na washabiki kadhaa wa klabu ya Yanga ya Jijini wameonesha wasiwasi na kutofurahishwa kufuatia ushindi alioupata Mwenyekiti mpya wa klabu ya Simba nayo ya Jijini, Juma Salum.

Juma Salum ameibuka tena kama Mwenyekiti wa Simba baada ya kuwabwaga wapinzani wake kadhaa katika uchaguzi uliofanyika Jumapili iliyopita Jijini Dar es Salaam. 

Baadhi ya wanachama na washabiki hao wamemueleza mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti Jijini kuwa hofu na wasiwasi walionao kwa Juma Salum unatokana na historia nzuri ya kiongozi huyo kuifunga Yanga. 

Historia inaonesha kuwa, Juma Salum aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Simba kuanzia 1989 mpaka 1993 na katika kipindi hicho, Yanga iliambulia kwa Simba sare na suluhu tu na ikibidi ushindi basi ni kwa mbinde tofauti na zama hizi. 

Kufuatia hali hiyo, kambi ya Yanga imekuwa ikihofia historia kujirudia baada ya Juma Salum kufanikiwa kukariri wadhida wake. 

Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi, Juma Salum alisema kuwa kazi ya kwanza iliyo mbele yake ni kuifunga Yanga ili kurejesha heshima ya Simba. 

Naye Kaimu Mwenyekiti wa Yanga, Abbas Tarimba alishindwa kabisa kuzungumzia suala hilo alipotakiwa na NASAHA na kumsukumia Katibu Mkuu Msaidizi, Mekline Kahigi ambaye hata hivyo hakupatikana mara moja. 


Mapunda asema hana bahati ya kutia mabao 

Na Mwandishi Wetu 

MSHAMBULIAJI hodari wa timu ya Simba ya Jijini, Steven Mapunda 'Garincha' amesema, kuwa hakuwa na bahati kabisa ya kuifungia timu yake pale ilipopambana na timu ya Majimaji ya Songea.

Mchezo kati ya timu hizo ulifanyika katikati ya wiki iliyopita katika uwanja wa Taifa jijini katika ligi kuu Tanzania Bara na Simba kupata ushindi wa bao 2-0. 

Katika mchezo huo, Mapunda alikosa mabao matatu ya wazi akiwa uso kwa uso na golikipa wa timu yake ya zamani ya Majimaji, Richard Mkongo aliyefuta mabao hayo. 

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Mapunda alisema, alishindwa kutumia nafasi hizo vema kwa kuwa hakuwa na bahati katika mchezo huo. 

"Nafasi nimezipata tena nzuri sana, lakini nimeshindwa kuzitumia vizuri, japo nilitumia uwezo wangu wote na hii inathibitisha kuwa sikuwa na bahati", amesema. 

Hata hivyo, Mapunda hakusita kuweka bayana kuwa kizingiti kikubwa katika mchezo huo alikuwa 'nyanda' wa Majimaji, Richard Mkongo aliyekataa kufungwa naye. 


Golikipa Majimaji alia na mabeki 

Na Mwandishi Wetu 

RICHARD Mkongo, golikipa wa timu ya Majimaji ya Songea amelalamikia kitendo cha walinzi wa timu yake kushindwa kupambana vilivyo na washambuliaji wa timu pinzani katika michezo ya ligi kuu Tanzania Bara.

Ametoa malalamiko hayo wiki iliyopita mjini Dar es Salaam mara baada ya mchezo kati ya Majimaji na Simba uliofanyika katika uwanja wa Taifa wilayani Temeke. 

Katika mchezo huo, Mkongo aliruhusu magoli mawili yaliyofungwa na washambuliaji wa Simba Shauri Iddi na Wicklef Ketto na kuokoa mengine matano ya dhahiri. 

Amesema kuwa Majimaji ingeweza kulazimisha suluhu katika mpambano huo kama walinzi wa timu hiyo wangekuwa imara kuwadhibiti watia mabao wa Simba. 

"Tatizo la timu yangu ni mabeki ambao hawachezi kwa ushirikiano katika kuokoa mashambulizi", ameongeza Mkongo ambaye alikuwa nyota siku hiyo. 

Juu
 

YALIYOMO
 

Tahariri
Wanaokemea dhuluma wasinyanyaswe

Waislamu waapa kuinyima kura CCM

Mkapa ahutubia Taifa: 
Ugumu wa maisha kuendelea

Wananchi wamuunga mkono Askofu Kakobe

MPASHO NASAHA
WAKIAMUA, HATA WAKICHAFUKA WATANAWA!!!

SHERIA
Faida ya kuwepo kwa sheria za haki kunategemea na wanaozisimamia

Ushauri Nasaha
Namna ya kumfanya mtoto wako aweze kuzungumza

MAKALA
Sababu ‘1000’ kwanini tunataka CCM ing’oke madarakani - 2

WAZO  LA  WIKI
Polisi acheni ubalakala

MAKALA
Kuporomoka kwa maadili  katika jamii yetu; Sababu na utatuzi wake - 2

Kalamu ya Mwandishi
Tatizo si jino kwa jino, bali utekelezaji muafaka!

MAKALA
Uchaguzi Mkuu Mwaka 2000 (6)
Vijana mjiandikishe kwa wingi na siku ya uchaguzi mjitokeze

Makala ya Mtangazaji
LEO NI SIKU YA ASHURA

Habari za Kimataifa

Riwaya
Kisasi cha mauti -3

Lishe
Ni kwa jinsi gani wanawake wanapata utapiamlo

MASHAIRI

MICHEZO

  • Madadi, Jamhuri acheni ‘rusha roho’ katika soka – Wapenzi
  • Yanga wakumbwa na kiwewe
  • Mapunda asema hana bahati ya kutia mabao

  • •••Golikipa Majimaji alia na mabeki 


       Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com

    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita