|
Na. 043 Jumatano Aprili 12- 18, 2000 |
|
|
|
|
|
LEO NI SIKU YA ASHURA MASAIBU
YA KERBALA
MUHARRAM Muharram ni mwezi wa kwanza (mwandamo) wa kalenda ya Kiislamu. Waislamu kote ulimwenguni
huadhimisha mwezi huu kwa huzuni kubwa kwa kumkumbuka Imam Husain (a.s.),
mjukuu wa Mtukufu Mtume Muhammad (s.a.w.w.) na Imam (kiongozi wa tatu wa
haki aliyeteuliwa na Mtume (s.a.w.w.).
ASHURA Siku ya mwezi 10 Muharram inajulikana kama ni siku ya Ashura. Imamu Husain (a.s.) aliuliwa kikatili pamoja na wafuasi wake wachache na ndugu zake. Masaibu haya yalitokea
zaidi ya miaka 1300 iliyopita huko Kerbala (karibu na mji wa Baghdad katika
nchi iitwayo Iraq hivi sasa).
IMAM HUSAIN (A.S.) ALIKUWA NANI? Chati inayoonyesha Nasaba ya familia ya Imamu Husain (a.s.):
HISTORIA KABLA YA MASAIBU Yazid, mtawala wa kimabavu (Dikteta) wa wakati huo, kusudio lake lilikuwa kuharibu na kuibomoa misingi ya Kiislamu. Utawala wake ulisababisha kutotosheka, rushwa na uvunjwaji wa sheria miongoni mwa Waislamu. Yazid alizikashifu na kuzivunja sharia za Kiislamu hadharani. Alikataza hata uhuru wa kimsingi wa kutoa mawazo na kuabudu na zaidi ya yote, alimtaka Imam Husain (a.s.) atoe baiya kwake, ambaye ni mjukuu wa mtukufu Mtume (s.a.w.w.) na kiongozi wa haki aliyeteuliwa. Jibu la Imam Husain (a.s.) kwa Yazid: Mtu kama mimi kamwe sitatoa baiya kwa mtu kama yeye (Yazid). Yazid alimtaka Imam Husain (a.s.) kutii amri yake vinginevyo angemuua. Imam alijibu: Sioni kifo
isipokuwa ni utukufu na kuishi na madhalimu ni mateso na ukandamizaji.
MASAIBU Imam Husain (a.s.) na wafuasi wake walipigana na jeshi la Yazid katika ardhi ya Karbala. Walinyimwa chakula na maji kwa muda wa siku 3 na hatimaye walichinjwa bila huruma. Miongoni mwa waliouawa shahidi alikuwa mtoto wa Imam Husain (a.s.) mwenye umri wa miezi 6 aliyeuawa kwa mshale wakati Imam Husain (a.s.) alipomuombea maji ili kukidhi kiu yake. Wanawake waliobakia walizungushwa
kutoka mji hadi mji na hatimaye walifikishwa kwenye mahakama ya Yazid na
kufungwa jela. Ushujaa kama ule wa Imamu Husain (a.s.) kamwe haukodhoofu.
Hakuna kati yao aliyesalimu amri kwa Yazid.
BAADA YA JANGA Masaibu yalizaa (yalileta) maisha mapya katika Uislamu. Yalileta mshituko na wasiwasi
katika Uislamu na mabadiliko ya hisia iliyosababisha, yaliimarisha wokovu
wa Imani.
MTAZAMO WA HULKA YA IMAM HUSAIN (A.S) Imam Husain (a.s.) ana sifa kama Qur'an tukufu inavyosema: Sema: Hakika sala zangu na matendo yangu ya maisha yangu na kifo changu. Vyote ni kwa ajili ya Allah muumba wa ulimwengu. (Qur'an 6:162). Katika ardhi ya Karbala kwenye dakika zake za mwisho Imamu Husain (a.s.) alisema: "...katika kukupenda Wewe (Ewe Allah) walau mwili wangu ungekatwa katwa vipande vipande, hata hivyo kichwa changu hakitomsujudia yeyote isipokuwa wewe Allah (s.w.t.). "...Iwapo hatima yangu ni kofi na kuoza mwili wangu, je ni kwa nini usikatwe mwili kwa ajili ya kutaka radhi yake Allah (s.w.t.). "...Iwapo Ujumbe wa Muhammad
hautabakia isipokuwa kwa kuuliwa mimi basi, Ee! Mapanga na yaje kuyatoa
maisha yangu."
MAFUNZO YA KUNUFAISHA Aliyekufa kwa ajili ya kuuhami Uislamu (shahidi) amefananishwa na mshumaa; ambao huteketea kwa ajili ya kuwaangazia nuru watu wengineo. Kujitoa muhanga Imma Husain (a.s.) tumepata nuru ya mwongozo hadi siku hii ya leo na nuru hii itaongoza milele na inamathili nadharia ya kujitolea, kutojinafisisha na kujitoa muhanga kidhati. Hii ndio sababu Waislamu
huhuzunika mwaka hadi mwaka, huendesha vipindi vya maombolezo, hupiga vifua
vyao na kufanya maandamano kwa jina la Imamu Husain (a.s.) hata baada ya
miaka 1300 tangu ya masaibu ya Kerbala.
MAISHA YA BAADAE (AKHERA) Usidhani kwamba wale waliouliwa katika njia ya Allah (s.w.t.) ni wafu (wamekufa). La hasha! Wao ni hai na Mwenyezi Mungu yupo pamoja nao, akiwaruzuku. (Qur'an 3:168). Kujitolea muhanga kwa Imam Husain (a.s.) ni uthibitisho wa dhati kuwa nguvu za kidhalimu sio zenye kufanikiwa daima. Alisimama imara kupinga vikali nguvu za magaidi wa wakati huo, kuulinda ukweli na haki ya binadamu na kuthibitisha kuwa Nguvu yake Allah (s.w.t.) wakati wote ni yenye kushinda udhalimu. Umma unawiwa deni la kiimani (kiroho) na Imamu Husain (a.s.). Yazid na wafuasi (jeshi lake) wameangamia, Imam Husain (a.s.) ataishi milele. KABURI LA IMAM HUSAIN (A.S.) HUKO KERBALA, IRAQ
|
YALIYOMO
Tahariri
Waislamu waapa kuinyima kura CCM Mkapa
ahutubia Taifa:
Wananchi wamuunga mkono Askofu Kakobe MPASHO NASAHA
SHERIA
Ushauri Nasaha
MAKALA
WAZO LA WIKI
MAKALA
Kalamu ya Mwandishi
MAKALA
Makala ya Mtangazaji
Riwaya
Lishe
•••Golikipa Majimaji alia na mabeki |
|
|
|
|