|
Na. 045 Jumatano Aprili 26 - Mei 2, 2000 |
|
|
|
|
|
S.L.P. 72045, Simu: 0811 - 600145, Dar es Salaam Acheni kuwacheza shere Waislamu, ondoeni udini Tangu Kadinali Pengo atangaze mpango wa Kanisa lake (Kanisa Katoliki) nchini kufuatilia uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, kumekuwepo na taarifa kadhaa katika vyombo mbalimbali vya habari nchini. Vikidai kuwa Waislamu wameulalamikia mpango huo wa Kanisa Katoliki. Katika habari hizo, imedhihiri kwamba mtazamo unaotolewa ni ule wa kuonesha hali ya Waislamu kuilalamikia serikali ili iwe sababu au kisingizio kwa Serikali kuchukua hatua ya wazi au ya kimyakimya kushinikiza Kanisa Katoliki kusitisha mpango wake huo. Tunaamini kuwa Serikali inataratibu zake za kufanya kazi na hatudhani kuwa taratibu hizo ni pamoja na kutumia mbinu za mzunguko mkubwa wa kipropanganda ili kufikia lengo lake. Kama kweli propaganda hizo za kutumia jina laWaislamu zina lengo la kuzuia mpango huo wa Kanisa Katoliki, bila shaka hakuna sheria yoyote iliyovunjwa na Kanisa Katoliki, katika kuweka mpango wale huo wa kufuatilia jinsi utakavyoendeshwa uchaguzi mkuu wa mwaka huu, pamoja na kuwaambia wanasiasa ni namna gani kanisa hilo linawataka waongoze nchi. Sisi pia tungependa kuamini hivyo, kwamba hakuna sheria yoyote iliyovunjwa na Kanisa Katoliki, kwa kuweka utaratibu wa kufuatilia uchaguzi mkuu wa mwaka huu nchini kuona kama utafanywa katika mazingira yaliyo huru na haki. Tunaamini hivyo kwa sababu Serikali yenyewe imekuwa kimya tangu Kanisa litangaze mpango wake huo. Aidha Serikali na chama kinachotawala (CCM) pia vimekuwa kimya mara nyingi Kanisa Katoliki linapo toa matamko ya kisiasa yanayo lenga kuisema Serikali, Chama tawala na hata baadhi ya viongozi wa juu katika utawala nchini. Na hayo pia tunaamini kwamba huwa hayavunji sheria yoyote. Lakini licha ya ukweli huo, Serikali siku zote imekuwa mstari wa mbele kuwakamata viongozi wa Kiislamu wanaposimama na kutoa maoni yao, au kuikosoa Serikali katika utendaji wake. Mfano mzuri ni kesi zinazo muandam Amiri wa Shura Sheikh Juma Mbukuzi kwa kutoa kauli za kuikosoa serikali. Mbali ya hayo yanayo muandama Sheikh huyo, Masheikh mbalimbali Mwanza, Arusha na Songea wamesikika wakiandamwa kwa visingizio vya "kuchanganya dini na siasa." Hapana shaka wanao waandama Waislamu wanajuwa kuwa wana wanawaonea na kuwadhulumu haki yao ya kidemokrasia na kikatiba. Haki ya kutoa maoni na kukosoa. Haki ambayo wananchi wenzao wa Kanisa Katoliki wana ruhusiwa kuitumia pasipo bughudha yoyote. Hivi karibuni pia wananchi wameshuhudia uhuru huo ukitumiwa vizuri na wenzao wa Makanisa ya Pentekosti, ingawa baadhi ya viongozi wa siasa nchini hawakutaka kuonesha kuwa Wapentekosti nao wana haki sawa na wenzao wa Kanisa Katoliki; jambo ambalo lililalamikiwa na waumini wa kanisa hilo pamoja na wananchi kadhaa wakiwemo Waislamu. Ni dhahiri lengo jingine la propaganda hizo za kutumia jina la Waislamu kama ni watu wanaolalamikia mpango huo, wa Kanisa Katoliki, ni mbinu ya kutaka kuonesha kuwa Waislamu wamekubali na kuridhia dhuluma ya kunyimwa haki ya kutoa maoni na kuikosoa Serikali; kwa dhana kwamba ipo sheria inayozuia uhuru huo. Lakini kwa mujibu wa kauli ya Amiri wa Shura ya Maimamu, Sheikh Jumba Mbukuzi kama ilivyo chapishwa katika gazeti hili, huo si mtazamo wala msimamo wa Waislamu. Kwa mujibu wa kauli ya Sheikh Mbukuzi, Waislamu wanaamini kuwa wanayo haki ya kutoa maoni na kuikosoa Serikali, tatizo ni Serikali kuwanyima haki hiyo pengine kwa sababu ya Uislamu wao tu. Ni kutokana na mtazamo huo, ndiyo maana Sheikh Mbukuzi anadai kuwa hilo nalo ni moja ya dhuluma za kiudini wanazofanyiwa Waislamu nchini. Kwa maana hiyo, si vizuri kwa baadhi ya watu na vyombo vya habari kutumia jina la Waislamu isivyo halali kwa ajili ya propaganda dhidi ya mpango wa Kanisa Katoliki kutaka kuona uchaguzi ujao unaendeshwa katika mazingira yaliyo huru na haki. Pamoja na udhaifu wa propaganda hiyo, bila shaka, lipo lengo la kuwabana Waislamu kabla ya wakati wa uchaguzi kwa hofu kwamba wao nao wasije na mpango kabambe wa kufuatilia utaratibu mzima wa uchaguzi mkuu ujao, ili kuona kuwa uadilifu unatendeka na dhuluma inakomeshwa katika uchaguzi huo. Kwa maana hiyo tungependa kuona wanaoendesha propaganda za kutumia
jina la Waislamu wanaacha. Kwani, propaganda hiyo ni sawa na kuwakebehi
kwa kuwacheza shere kwamba, wenzao Wakatoliki wameruhusiwa na wao walie
tu. Huo nao ni udini unaostahili kuondolewa.
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Serikali iache udini, kuwagawa wananchi - Sheikh Mbukuzi Wakati
Kanisa Katoliki likitoa miongozo ya kisiasa:
Hakuna maendeleo bila Demokrasia - Lipumba MPASHO NASAHA
HABARI
‘Suala la kuirekebisha jamii lisiachwe mikononi mwa Serikali pekee’ Jiandikisheni na pigeni kura -Balozi Tanzania
kufutiwa madeni:
Ushauri Nasaha
MAKALA
Kalamu ya Mwandishi
MAKALA
Lishe
RIWAYA
|
|
|
|
|