NASAHA
Na. 065 Jumatano Septemba 13 - 19, 2000
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
MASHAIRI


Ngangari inameremeta

Hodi hodi uwanjani, Sabaya nipe kalamu,
Nataka kuwapasheni, hakika muifahamu,
Baby Fumo pita ndani, mkombozi Mariamu,
Inameremeta sana, Lipumba nuruye sana. 

Nuru haitoki mbali, Tabora si Ukaguru,
Imechomoza miali, si kwengine Lolanguru,
Msitafute muhali, si Mtwara si Luguru,
Inameremeta sana, Lipumba nuruye sana. 

Nuru uchumi “ngangari”, kichwani umetulia,
Nuru siasa “ngangari”, mahiri kupindukia,
Nuru haitakabari, Ikulu ikiingia,
Inameremeta sana Lipumba, nuruye sana. 

Nuru yatikisa miti, miamba na majabali,
Nuru imejizatiti, vikongwe wako chakali,
Nuru sio afriti, “Bwana Madeni” muhali,
Inameremeta sana, Lipumba nuruye sana. 

Nuru sasa inavuma, Kikongwe anachachawa,
Nuru imeteka umma, namba wani kapagawa,
Nuru hairudi nyuma, yenda mbele maridhawa,
Inameremeta sana, Lipumba nuruye sana. 

Shime ndugu zangu shime, nuru yetu tuienzi,
Namba wani tuinyime, ikose kiti cha enzi,
Hata roho ziwaume, nuru ndo yetu kipenzi,
Inameremeta sana, Lipumba nuruye sana. 

Kaditama namaliza, ngangari wote vipenzi,
Mwiko nuru kufifiza, Oktoba tuienzi,
Nambawani kunagiza, watatukwea makonzi,
Anameremeta sana, Lipumba huyo ngangari. 

Na Juma S. Katanga (JUSHAKA) 
S.L.P. 872 
Mapumzikoni 
(Mwishowanchi) - Kigoma



Sera za kweli

Bismillahi Rahimu, kwa jina lake Manani,
Salamu Alaykumu, mhariri nasahani,
Nina khabari muhimu, naomba unisaini,
Wana-CUF ni ngangari, kwa sera zao za kweli. 

Khutuba zake Lipumba, zinaingia kichwani,
Akinena mwana Yomba, husherehesha makini,
CUF dume watalamba, Oktoba karibuni,
Wana-CUF ni ngangari, kwa sera zao za kweli. 

CCM yanyanyasa, na waumini nchini,
Wanaua kama kasa, damu yamwagika chini
Na mpige yule khasa, yule kamuweke ndani,
Wana-CUF ni ngangari, kwa sera zao za kweli. 

Wakati wakaribia, kuingia chaguzini,
Tusije tukarudia, makosa yetu mwanzoni,
Tukusudie kwania, kuiaga namba wani,
CCM baibai, twakuaga buriani. 

Lipumba Sefu Sharifu, nawaomba tulieni,
Pasiwe wasi na khofu, sera zenu enezeni,
Kiongozi wetu CUF, elufu mbili mwishoni,
CCM kwa herini, hatukutakeni tena. 

Beti sita nimefika, kalamu naweka chini,
Kitini ninainuka, nakwenda zangu shambani,
Huenda nikafarajika, na maisha haya duni,
CCM mmeoza, dawa ni kukuzikeni. 

Ustadhi Seifu Omari, 
S.L.P. 100054, 
Dar es Salaam.



Maisha

Amina lete kalamu, na karatasi mezani,
Na tena fanya muhimu, nataka kwenda shambani,
Sada Vumi na Mshamu, Nyambi njooni uani
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Tamaa si kitu chema, wanangu nawambieni,
Yangu muyashike vema, msije fanya utani,
Ya sasa sio ya zama, Dunia yenda mwishoni,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Tamaa huleta kilio, mijini na vijijini,
Fungueni masikio, yangu muweke kichwani,
Sio tu ndio ndio, mkaniona punguani,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Wapo walio wengi, sasa wameshapotea,
Kisa ni kuvuta bangi, na mapombe kujinywea,
Wengine ni mashangingi, ukimwi wanaugua,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Nisemayo si upuuzi, huu ni wangu wasia,
Mkija kufanya wizi, moto mtajaungua,
Na kama ni ujambazi, risasi zitawaka,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Kuna mengi ya hatari, msifanye masihara,
Mkijakuwa taperi, mtaja ozea jera,
Zitulizeni akiri, acheni zenu papara,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Nasema someni wana, elimu kupigania,
Msijefanya hiyana, maisha mtajutia,
Msiendekeze ujana, ujana wapita njia,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Kaditamati watama, hapa ninaishilia,
Nakimbilia kulima, mvua inakaribia,
Na nyinyi fanyeni hima, kengere imeshalia,
Maisha kushinda moyo, tamaa si kitu chema. 

Mnyonge wa haki, Kasimu J. Ndava, 
S.L.P. 100054,
 Mbagala.

Juu
 

YALIYOMO
 

TAHARIRI
Tume, kauli ipi sawa? 

CCM maji shingoni 

Wazanzibar wawaambia Dk. Omar na Karume:
Kura tutawanyima, mtang’oka 

CCM ni nguruwe aliyenona - Mtopea 

Kabobe asisitiza uchaguzi huru 

Mkapa aomba kura kwa hoja ya uzawa 

Vifaa vya uchaguzi vimeanza kusambazwa 

Mizengwe yatupwa,wagombea upinzani wapeta 

HABARI ZA KIMATAIFA

USHAURI NASAHA
Haya ndiyo mambo ya wanawake - 2 

MAKALA
Kura ni silaha 

Kampeni za uchaguzi Zanzibar zimetosha kumvua chui ngozi ya mwana kondoo 

MPASHO NASAHA
BEN NA BULLY 

MAKALA
Wimbo wa Umoja na Amani wa CCM  ni ghilba za kisiasa 

KALAMU YA MWANDISHI
Hojini Ubalozi wa Vatican kwanza 

MAKALA
CCM kushinda uchaguzi bila kupigiwa kura? 

MAKALA
Mwenye macho haambiwi tazama - 4 

CUF Tanga wamsihi Mufti wa BAKWATA aachane na siasa 

Kodi ya Maendeleo haitaondolewa -Mkapa 

Wazee waijibu CCM 

BARUA

MASHAIRI

MICHEZO

  • Yanga watakiona - Kajumulo
  • Simba yajaribu kombe la FAT
  • Tarimba akataa ubabe
  • Jeshi laongeza timu Ligi Kuu

  •  

       Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com

    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita