|
Mashairi
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani (jibu la
mwokozi Yesu)
Bwana Dettu tafadhali, soma Biblia yakini,
Niwapi Yesu kakili, kwitwa NENO na Manani,
Mmemzulia Jalali, Neno kuwa Yesu tubuni,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Tubuni kabla ya Kiama, Yesu mwenyewe kasema,
Moja tatu Luka soma, katika mbili nne soma,
Tatu sifuri ukoma, tajua wenye hekima,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Yesu kwanza kazaliwa, Mamaye ni Mariyamu,
Tamshi lilitolewa, hakuumbwa kama Adamu,
Umasihi akapewa, alete kwa wanadamu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Kaumba kwanza Adamu, bila baba wala mama,
Hawa naye binadamu, kaja bila mama soma,
Yesu mamaye Maryamu, naye kapewa neema,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Mungu anayo hekima, hanaye wa kufanana,
Yesu dume tumesoma, vipi Mola kulingana,
Isaya nne sita soma, laini tano taona,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Mungu hana mshirika, Manabii walisema,
Hata Yesu kasikika, Isaya naye kasema,
Aya nne tano hakika, tano hadi saba soma,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Yesu alipotundikwa, alomba msalabani,
Baba yetu mkumbukwa, nondoshee mtihani,
Usinache nikafikwa, na kifo msalabani,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Yohana moja na moja, hadi sita ulosema,
Hayo si ya Mola mmoja, bali ya watu nasema,
Mola hamwambii mja, maneno yasohekima,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Yesu kasema katumwa, wewe wamwita Mungu,
Moja saba imesema, Yohana tatu kirungu,
Mungu mmoja imetemwa, Yesu nawe nani Mungu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Yesu hasemi uongo, kuwa na yeye ni Mungu,
Yohana mbili mzingo, moja saba soma ndugu,
Kweli tabaini pengo, sote baba yetu Mungu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Memzulia uongo, kuwa mwokozi mkuu,
Tito mbili yaulongo, moja tatu hadi kuu,
Yohana moja nne tengo, mbili nane nanukuu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Vitabu vyote vya Mungu, hasa vilivyo sahihi,
Katika ardhi na mbingu, Muumba Mola walahi,
Viumbe vya ulimwengu, hakuna wakukebehi,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Dettu kwanza tafakari, kama kweli Yesu Mungu,
Kwa makini ufikiri, nani alitoa fungu,
Yesu ndani ya kaburi, siku tatu bila Mungu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Dettu sisi twamini, Mungu wa Yesu na wote,
Manabii duniani, aliwatuma walete,
Mungu moja tuamini, hana mshirika kote,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Hajatokea Nabia, tangu Mtume Adamu,
Tamati wa Arabia, eti mwana wa Maryamu,
Mkombozi wa dunia, hakika Mungu hakimu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Siku kiama kikija, Mungu kutoa hukumu,
Utajaona kioja, kumbe Yesu Mwisilamu,
Kanisa hakulionja, kaketi na Ibrahimu,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Hapa pangu kituoni, kalamu naweka chini,
Dettu soma Kuruani, ukweli utabaini,
Uache uhayawani, utakwisha motoni,
Mwokozi Mwenyezi Mungu, siyo Yesu asilani.
Juma Hassan,
P.O. Box 70026,
Ubungo, Dar es Salaam.
Mtukufu Ramadhani
Bismilahi Raufu, Mhariri gazetini,
Mimi sio maarufu, hapo kwenu kilingeni,
Nataka kuwaarifu, Islamu na Misheni,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Mwezi huu mtukufu, jina lake Ramadhani,
Utende matakatifu, ninatoa ilani,
Utapata utukufu, mwisho wake duniani,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Najaribu kuhubiri, bado kupata yakini,
Imekuwa desturi, ifikapo Ramadhani,
Kutuuzia futari, bei juu magengeni,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Mwezi huu mashuhuri, asiyejua ni nani?
Biashara hushamiri, dukani hata sokoni,
Yafaa ujihadhari, unapo uza sokoni,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Kiumbe fanya nadhari, bei ziwe wastani,
Usitake utajiri, kudhulumu maskini,
Watu wote si tajiri, wanunuao sokoni,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Imekuwa staili, ifikapo Ramadhani,
Bei zenu kubadili, sokoni na madukani,
Bidhaa kuuza ghali, hata haya hamuoni,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Natoa hii kauli, AN-NUUR gazetini,
Wasikie Waswahili, walio bara na pwani,
Lanikera jambo hili, tumugope Manani,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Huo ndio ukafiri, mimi nawaambieni,
Kudhulumu mafakiri, waliojaa madeni,
Hii kweli sio siri, mimi sijui kwa nini?
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Mohammadi na kakiri, huko kwao Arabuni,
Alizifanya safari, akiwa biasharani,
Aliuza kwa kadiri, hakufanya uhaini,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Katitamati shairi, Mhariri samahani,
Mungu atakusitiri, uiendeleze fani,
Na akujaze na heri, upate nishani,
Mwezi huu Mtukufu, kiumbe wacha dhuluma.
Ustadh Abdallah Aziz (Darigube)
Masjid Qiblatain English Medium Primary School,
DAR ES SALAAM.
|
YALIYOMO
Tahariri
Umaskini unachafua mazingira!
Mauaji ya
Mwembechai: Spika wa Bunge aombwa atoe gharama za kuunda Tume
UWAWARU
yafa Rufiji
UN yaidhinisha
udhalimu wa Marekani
Qur’an
yachomwa moto Shinyanga
Marekani
yadhihirisha Ubeberu wake
MARADHI
YA KISAIKOLOJIA: SEXUAL SADISM
Na. Abu Halima Sachangwa
Kitengo
cha Zaka chazinduliwa Dar
Tume
ya Jiji kubomoa Msikiti wa vipofu
Akheri ya
zamani
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington
DC. USA
UWAWARU
yaleta nusura Ikwiriri
Tamko
la Masjid NNUUR juu ya kuanzishwa kwa UWAWARU
Kuanzishwa
kwa UWAWARU
Wasomi
Waislamu wawajibike
Na Mwandishi Wetu
Albucasis
936 - 1013 (CE)
Ijue
Uhuru madrasa - Morogoro
Madrasa
Akhlaqil Islamiya yapiga hatua
MADRASATUL
Husseiniyi Shadhily
Na Jamillah Nassoro
Hatimaye
kesi ya kushambulia kituo nayo yafutwa
Changieni
vyombo vya mihadhara - Sheikh Said
Misikiti
yakosa maji ya kutawadhia
Bakwata
Tanga haifuati katiba yake
Sheikh
Mbukuzi ataka Waislamu watafute radhi za Allah
Je,
hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? - 3
Na Mwinjilisti Bunga E.
Dettu
Njia
ya uzimani ni nyembamba, waionao ni wachache - 3
Na Yasin Valerian Massawe
Sheikh
Omar Bashir afikishwa mahakamani
Mufti
pekee kuidhinisha watu kufunga
Nguruwe
wanaofugwa maeneo wanayoishi watu kusababisha magonjwa ya kuambikiza
200
wamesilimu
Sayansi
na Teknolojia
[Kuiweka Modem kwenye Kompyuta]
Masomo
ya Dini ya Kiislamu
Barua
za Wasomaji
Mashairi
Chakula
na lishe
[Mlo wa Daku]
Tangazo
New Book: The untold story
of the Muslim struggle against British Colonialism in Tanganyika. |