NASAHA
Na. 082 Jumatano Januari 10 - 16, 2001
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
HABARI ZA KIMATAIFA 
 

Upinzani kuondoa uozo wa chama tawala

ACCRA, Ghana.

SHEREHE za kumuapisha Rais mpya wa Ghana, Bwana John Kufuor, zimefanyika wiki hii na hivyo kuanza kazi ya kuondoa matatizo ya kilichokuwa chama tawala.

Akizungumza baada ya kuapishwa, Bwana John Kufuor amesema kazi kubwa ya serikali yake ni kuepuka maovu yote yaliyofanywa na serikali iliyopita ya Bw. Jerry Rawlings. 

Ameahidi kuboresha uchumi, huduma za jamii, kuondoa rushwa, ufisadi na uzembe. 

Ameongeza zaidi kuwa atafanya kazi kwa uadilifu kwa manufaa ya wananchi. 

Bwana Kufuor ameahidi kumheshimu Bwana Rawlings kama Rais Mstaafu kwa kumpa hadhi inayostahiki. 

Naye Bw. Rawlings wiki iliyopita alimaliza wadhifa wake kwa kukagua gwaride la kijeshi huku akiwa amevalia vazi la kijeshi. 

Amesema, anaondoka madarakani huku akijua kuwa uchumi umeboreka zaidi kuliko pale alipoingia madarakani kwa mapinduzi mnamo mwaka 1981. 

Bw. Rawlings anatarajiwa kupokea na kukubali wadhifa wa ubalozi aliotunukiwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Koffi Annan. 

Kwa wadhifa huo atakuwa akizitembelea nchi mbalimbali katika shughuli za kidiplomasia. 


Jaribio la mapinduzi shughuli nzito yaendelea 



ABIDJAN , Ivory Coast.

MAPINDUZI huko Ivory Coast yamekwama hapo juzi baada ya askari watiifu wa serikali kuzima jaribio hilo.

Waziri Mkuu wa nchi hiyo alitangaza kuwa jaribio hilo lilifanyika usiku wa kuamkia juzi ambapo askari watiifu wa serikali iliyopo madarakani walizima mapinduzi hayo. 

Milio na milipuka ilisikika kutoka usiku hadi alfajiri katika kurupushani hiyo ambapo baadhi ya nyumba karibu na vituo vya Redio na Televesheni ya Taifa zilipata mtikisiko, ameeleza mkazi mmoja jirani na kituo cha TV katika wilaya ya Kokodi. 

Imedaiwa kuwa waliofanya jaribio hilo ni wapiganaji wa Jenerali Robert Guei ambaye alitimuliwa madarakani hapo mwaka jana katika jaribio la kuchezea kura za wananchi. 

Katika kinyang'anyiro hicho cha Rais Bw. Laurent Gdabo alikwaa madaraka huku akiwatimulia vumbi washiriki uchaguzi akina Alasdne Ouatara aliyependwa na wananchi wengi nchini humo. 

Habari zaidi zimeeleza kuwa katika mapigano kati ya vikosi vya serikali na wanamapinduzi, Maafisa Usalama wa serikali wawili wameuawa na kwa upande wa pili wanne wamepoteza maisha. 

Wanamapinduzi walishikilia kwa muda vituo vya televisheni na radio kabla kunyang'anywa na vikosi vya serikali. 

Rais Laurent Gdabo amelielezea tukio hilo kuwa ni kitendo cha ugaidi. Rais huyo hakuwepo nyumbani kwake mjini hapo, alitarajiwa kurudi jana toka kijijini kwake. 

Wachunguzi wa kisiasa wamesema kuwa jaribio hilo inaonesha kuwa shughuli nzito inaukabili utawala wake ikizingatiwa kuwa naye ameingia madarakani kwa mizengwe ya kumzuia Bw. Alasane Outara asigombee uongozi wowote nchini humo. 

Zoezi hilo alilorithi toka kwa Guei aliyetimuliwa, naye aliwazuia kwa mbinu watu kadhaa wasigombee Urais hatimaye kuchezea kura za wananchi walioshirikiana na Bw. Outara kumuondoa mbio na Gdabo kukwaa madaraka kwa kukataa kurudia uchaguzi. 


Hizbullah watoa mkong'oto 

BEIRUT

KIKUNDI cha wapiganaji wa Kiislamu, Hizbullah wiki hii wameendelea kupambana na Israeli katika tambarare za Sheba. 

Wapiganaji hao waliopo Lebanon wamesema wanapambana na Israeli ili kurudisha ardhi iliyoporwa zaidi ya miaka hamsini iliyopita. 

Huku wakiungwa mkono kwa hali na silaha kutoka Syria, Iran na nchi nyingine za Kiislamu wapiganaji hao wameeleza kuwa kujitoa kwa Israeli mnamo mwaka jana katika baadhi ya maeneo hakutoshi hadi hapo milima ya Golan iliyopo Syria na sehemu nyingine ziachwe kukaliwa kwa mabavu na walowezi hao wa Kiyahudi. 

Israeli iliyavamia kijeshi maeneo ya nchi za Syria, Lebanon na Palestina na kuyakalia kimabavu zaidi ya miaka 52 iliyopita. 

Katika juhudi za kurudisha ardhi iliyotekwa, kikundi cha Hizbullah kilianzishwa mnamo 1982 ambapo mnamo mwaka uliopita walizidi kutoa mkong'oto hadi Israeli wakaachia baadhi ya maeneo. 


Katiba ya kijamaa yabomolewa 



SENEGAL

MAONI ya mabadiliko ya katiba yanafanyika wiki hii nchini Senegal katika upanuzi wa demokrasia.

Mabadiliko hayo yanasimamiwa na kuongozwa na chama cha upinzani kilichoingia madarakani mwezi Machi mwaka uliopita baada ya kukimbwaga chini chama tawala. 

Katika marekebisho hayo kuna mpango wa kupunguza kipindi cha Rais kuwa madarakani kutoka miaka saba hadi mitano. 

Aidha Rais atatakiwa kudumu kwa vipindi viwili tu vya miaka mitano kila kimoja. 

Katiba pia itampa nguvu rais kumchagua na kumfukuza kazi Waziri Mkuu. 

Wanawake nchini humo watafaidika na mabadiliko hayo kwani pamoja haki zingine zaidi wataruhusiwa kisheria kumiliki mashamba (ardhi). 

Mabadiliko zaidi yanatarajiwa kufanyika katika maoni ya kubomoa katiba hiyo ambayo toka nchini hiyo ilipopata uhuru miaka 40 iliyopita ilikuwa inahodhiwa na chama cha Kisoshalisti chini ya Bwana Abdou Djiouf. 

Kufuatia upinzani kushinda katika uchaguzi wa mwaka jana na hivyo kumuweka madarakani Rais Abdilouye Wade hivi sasa juhudi zinafanywa kurekebisha masuala ya utawala ili kuwa na uongozi bora. 


Kampeni ijayo uchumi -Blair 

LONDON, Uingereza.

KATIKA kipindi cha uchaguzi kijacho mkazo utakuwa katika uchumi zaidi.

Hayo yamesemwa na Waziri Mkuu wa nchi hiyo Bwana Tony Blair, kiongozi wa chama cha Labour wakati akiongea na kituo cha televisheni cha BBC.

Amefanunua kuwa katika kampeni za uchaguzi, uchumi utapewa kipaumbele kwa kuhakiki kazi ya kuboresha uchumi iliyofanywa na Labour pamoja ma mikakati ya kuboresha zaidi kipindi kijacho. 

Hata hivyo hakuweleza uchaguzi mkuu utaitishwa lini, japokuwa inatarajiwa utafanyika mapema kwa sababu ya uhakika wa kuongoza katika kura za maoni kutoka kwa wananchi juu ya imani kwa serikali yake. 

Wakati huo huo, Bwana Blair anatarajiwa kwenda Marekani mwezi ujao, pamoja na kwenda kumpongeza Bw. Goerge W. Bush kwa kuwa Rais wa 43 wa taifa hilo zaidi ni kuimarisha ushirikiano wa chama cha Labour na Repubnlican. 

Ziara hiyo inatarajiwa kufuata propanganda zilizoenea kuwa Bw. Blair hatatoa ushirikiano endapo Bwana Bush angeshinda kunyang'anyiro cha Urais. 


Spika anusurika kutekwa



MOGADISHU, Somalia.

SPIKA wa serikali mpya ya Somalia ameponea chupu chupu kutekwa nyara.

Moaofisa wa serikali wamesema kuwa watu wenye silaha kali walifanya jaribio hilo ambapo walinzi wa Spika walifanikiwa kuzima jaribio hilo. 

Spika huyo wa serikali hiyo ya mpito Bwana Abdallah Deroh Isaaq yuko katika hali salama. 

Hadi sasa hazijafahamika sababu za kufanywa na kikundi cha RRA cha nchini humo. 
 

Juu
 

YALIYOMO
 

MAONI YETU
Mapinduzi Zanzibar yameleta kilichokusudiwa?

Wananchi wamwambia Mkapa:
Mbumbumbu wa demokrasia waliomo katika chama tawala ni hatari zaidi

Waislamu watakiwa kuwa watekelezaji wa maamuzi

‘Hajj Trust’ yaongeza huduma kwa mahujaji

DONDOO MUHIMU

MAKALA
Jamii ijihadhari viongozi wasaliti

MAKALA
Msimamo wa Pengo haushangazi

KALAMU YA MWANDISHI
Kitendawili cha millenia: Urais bila dola

MAKALA
Dhana ya kumwabudu Mungu anayeafiki udhalimu lazima tuikatae

MAKALA
Mapinduzi Zanzibar: Dhuluma bado ipo

MAKALA
CCM haiwezi kuondosha umasikini Tanzania

MAKALA
Tirivyogo la sekta ya elimu

Mwenye Macho……
Demokrasia haiwezi kujengwa kwa kuvunja katiba

HABARI ZA KIMATAIFA

MASHAIRI

MICHEZO

  • Baadaya Mkapa kushindwa kusaidia: Prof. Lipumba aombwa kuiombea Tanzania FIFA
  • Mtwa aanza kulala mapema
  • Salvatory aitwa Mtibwa

  •    Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com

    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita