NASAHA
Na. 035 Jumatano Februari 16 - 22, 2000
Ukurasa wa mwanzo
Islam Tanzania
Matoleo yaliyopita
Wakati Rais Mkapa apinga kuwepo kwa dhuluma dhidi ya Waislamu:
Wanafunzi wa Kiislamu shule za sekondari za serikali Dar wanyanyaswa 
  • Wakatazwa kuhudhuria khitma iliyoandaliwa na Halmashauri Kuu ya Waislamu 
  • Watishwa majina yao yatapelekwa katika vyombo vya dola 
  • Wazazi watafakari vitisho dhidi ya watoto wao 
Na Mwandishi Wetu

WAZAZI wa wanafunzi wa Kiislamu katika baadhi ya shule za sekondari za serikali jijini Dar es Saaam wameilalamikia hatua ya shule hizo kuwazuia wanafunzi wa Kiislamu kushiriki hafla za kidini na kutoa vitisho ambavyo vitawafanya wawe wakisoma kwa hofu hali ambayo wamesema itaathiri matokeo yao kitaaluma.

Imeelezwa kuwa katika shule ya sekondari ya Kisutu, jijini Dar es Salaam, wanafunzi kadhaa wa Kiislamu waliitwa na uongozi wa shule na kisha kuhojiwa siku za Ijumaa na Jumatatu kufuatia kuonekana tangazo lilobandikwa shuleni hapo kuwaalika Waislamu kuhudhuria khitma ya kuwaombea dua Waislamu waliouawa Mwembechai. 

Wazazi wa wanafunzi wa Kiislamu waliohojiwa na timu ya waalimu wameliambia gazeti hili kwamba watoto wao walihojiwa maswali ambayo wao wanaamini hayakuwa na sababu yoyote kitaaluma na wala kiutawala. 

Bw. Masoud, mmoja wa wazazi hao amesema miongoni mwa maswali waliyoulizwa ni nani kati ya Sheikh Ponda na Sheikh Mbukuzi angehutubia. 

Kwa mujibu wa mzazi huyo baada ya kuhojiwa siku ya Ijumaa, Februari 11, wanafunzi hao waliitwa tena kuhojiwa siku ya Jumatatu Februari 14, siku moja baada ya kufanyika kwa khitma hiyo ambapo waislamu wote walikuwa wamealikwa. 

"Walimu hawa hawakuchoka hata kidogo. Mahojiano ya Ijumaa hayakuwatosha, wakawasalisha (wakawahoji) tena jana Jumatatu. 

"Eti wamewauliza, 'wangapi mlihudhuria khitma'; tajeni wanasheria waliozungumza; 'Ponda alisema nini; (Ponda) alipoingia mlishangilia kwanini?" alisema mzazi huyo. 

Mzazi mwingine alisema ameshangazwa na hatua hiyo ya shule ya Kisutu kuwazuia wanafunzi wa Kiislamu kuhudhuria khitma hiyo iliyoandaliwa na Halmashauri Kuu ya Waislamu ambayo inatambuliwa na Rais na imekuwa ikifanya mazungumzo na Rais Mkapa juu ya dhuluma wanazofanyiwa Waislamu na serikali. 

Mzazi huyo ambaye hakupenda kutajwa gazetini alisema, "kuwatisha wanafunzi wasihudhurie khitma ni kuwazuia wasifanye mambo ya ibada zao. Isitoshe khitma yenyewe ilikuwa Jumapili, (siku hiyo) hakuna kazi wala shule sasa kikwazo ilikuwa nini kama sio uonevu?" 

Aidha sekondari ya Kisutu ni shule ya kutwa ambapo wanafunzi hawalali shuleni. 

NASAHA ilipotaka kujua vitisho walivyopewa wanafunzi hao, mzazi huyo ambaye alijitaja kuwa ni afisa mstaafu serikalini alisema kwamba wanafunzi hao waliambiwa kuwa maelezo yao waliyoyatoa kwa walimu hao, majina yao na mahali wanapoishi vitapelekwa katika vyombo vya dola. 

Aidha wazazi hao wamesema wanakusudia kuwaona viongozi wa HALASHAURI Kuu ya waislamu ili suala hili walipeleke kwa Mh. Rais kama ushahidi wa unyanyasaji dhidi ya Waislamu. 

NASAHA ilibahatika kuzungumza na baadhi ya wanafunzi wa Kiislamu wa shule hiyo ambao waliieleza kwamba wamekuwa wakitakiwa wasijihusishe na jumuiya ya wanafunzi wa Kiislamu katika shule za sekondari za mkoa wa Dar es Salaam DAMUSSA. "...wanatuambia (kuwa) DAMUSSA siyo nzuri kwetu na wakati mwingine viongozi wake (DAMUSSA) huwa wanazuiliwa wasiingie shuleni hapa", alisema mwanafunzi mmoja wa kidato cha tatu. 

Mwanafunzi mwingine wa Kiislamu alimuunga mkono mwenzie na kuongeza kuwa kizuizi hicho hawakioni kwa jumuiya za wanafunzi wa Kikristo kama vile UKWATA na TYCS. 

"Viongozi wa UKWATA na TYCS wanakuja hapa kila mara kuzungumza na (wanafunzi) Wakiristo, lakini sio DAMUSSA", alisema mwanafunzi huyo. 

Juhudi za gazeti hili kuzungumza na uongozi wa shule hiyo hazikuzaa matunda kwa maelezo kuwa wasemaji wa suala hilo hawakuwepo. 

Mwalimu mmoja ambaye hakukubali kutajwa gazetini aliwataja walimu wenzake ambao wanaweza kuzungumzia suala hilo kuwa ni Mkuu wa shule Msaidizi, Mama Shaba, Mwalimu wa Taaluma, Mama Kilama, Mwalimu Mlezi wa wanafunzi Waislamu, Mama Issa na Mama Nzingo kwa vile wao ndio walihusika kuwahoji wanafunzi hao. 

Juu
 

YALIYOMO
 

Tahariri:
Serikali itoe hatma ya mauaji ya Mwembechai 

Wanafunzi wa Kiislamu shule za sekondari za serikali Dar wanyanyaswa 

Kanisa liliishinikiza serikali-Waislamu

Sakata ya mabadiliko ya Katiba Zanzibar 

Kukiri kosa na kuomba radhi ndio kipimo cha utu 

HABARI ZA KIMATAIFA 

Ushauri Nasaha  
Kuongoza tabia za watoto 

MAKALA 
Uhuru wa pili na ukombozi wa mwananchi 

MAKALA 
Umuhimu wa uchumi katika Uislam 

Kalamu ya Mwandishi 
Kwa nini kadhia ya Mwembe Chai isifanyiwe uchunguzi? 

Makala 
UPINZANI  OCTOBA 2000 - 3 

MAKALA
MAREKEBISHO YA 13 YA KATIBA YA  JAMHURI YA MUUNGANO: Wananchi Tanzania amkeni 

Riwaya 
Ndoto ya mafanikio 

LISHE 
Vyakula vitupatiavyo mafuta 

Barua/Maoni

MASHAIRI

MICHEZO

  • Tauzany afurahia ligi ya makundi 
  • Kibadeni hakutokomea na fedha za usajili- Milambo 
  • FAT yamuangukia Gama

  •  

     


       Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:Bonyeza hapa
    Au
    Andika barua  kwa: nasaha1420@yahoo.com


    Ukurasa wa mwanzo
    Islam Tanzania
    Matoleo yaliyopita