|
MASHAIRI
Utenzi wa Kongamano la akinamama Tanga
Hodi hodi Mhariri, Naingia kwa fakhari,
Niseme yaliyo kheri, Yawafae Islam.
Salam nakutolea, Ilojaa nyingi dua,
Na Rehma za Karima, Nazitoa kwa jamia.
Wageni mlofikishwa, Tanga tumefurahishwa,
Katu hatutayumbishwa, Msimamo twawapasha.
Walisema halitawa, Mbona sasa limekuwa,
Vitisho na nyingi mbawa, Wanawake kufanyiwa.
Ni askari wa dola, Wasomuogopa Mola,
Walotanda kila kola, Na maswali kutudanda.
Kibali kuulizia, Kutafuta kutuzuia,
Kuivunja yetu nia, Wanawake kukutana.
Mola wetu kajalia, Kuepusha zao hilo,
Kongamano limekua, Mawazo tumepeana.
Tumeonewa vyatosha, Kilobaki twawapasha,
Katu hatutabakisha, Tutasema vyakutosha.
Waislamu wanawake, Shime tuunganike,
Tusije fanya makeke, Adui kutuhadaa.
Tusijefanya ajizi, Tukawaiga washenzi,
Tabia na lao vazi, Vitatuangamiza.
Tuvae nguo stara, Zile zisizo na dhara,
Ni jadi yetu stara, Kuiga hakutufai.
Tusimkosoe Manani, Dawa ya ngozi ya nini,
Mwajichubua kwa nini, Mola tunamchukiza.
Tujielimishe kidhati, Madada na wetu binti,
Tusipoteze bahati, Allah atatuuliza.
Tusikubali dhuluma, Ikibidi tutasema,
Sasa basi tunasema, Kuonewa hatutaki.
Mwembechai ni mfano, Hatulisahau mno,
Waliokufa mfano, Tuliobaki radhi kufa.
Kamwe tusiwe wazito, Duniani ni mapito,
Tusiwe kama watoto, Kongamano twaagiza.
Wenzenu Tanga twasema, Kosa hatutorudia,
Elfu mbili kufikia, Kweli tutaionyesha.
Haki
Haki ipo popote wajibu, kwa waja kutimiziwa,
Vimeandikwa vitabu, ambavyo tumeshushiwa,
Ameagiza Wahabu, pasiwe kudhulumiwa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Haki neno hili haki, si neno la kuchezewa,
Husababisha hamaki, wapewa wasipopewa,
Huzusha kutaharuki, na madhara kuchochewa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Watu hutumia nguvu, haki ikihujumiwa,
Purukushani – mabavu, huenda yakatumiwa,
Ukakoma ulegevu, haki yao kupatiwa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Haki mithili ya boya, kwa waliokusudiwa,
Haiko kama hidaya, ya mtu kuzawadiwa,
Kuikosesha vibaya, mwisho ni kuadhibiwa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Haki iwe ya ye yote, hakuna kubaguliwa,
Ni lazima aipate, japo ni kwa kuchelewa,
‘Dhulumati’ asiote, kwamba atanusurika,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Haki jambo hili zito, yatakiwa kutetewa,
Ya kauli ama pato, isiwe kubadilika,
Chumo la dhambi majuto, kwa wale watuhumiwa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu
Haki ikikosekana, kwa waliodhamiriwa,
Salama huwa hakuna, ‘woga’ watu huishiwa,
Huwa radhi kupambana, si kingine kusikiya,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Nafanya ufupishaji, shairi latamatiwa,
Natulia nataraji, ujumbe umesikiwa,
Ndimi mwana wa Miraji, Kassim mwenye kipawa,
Haki ikidhulumiwa, huchukuliwa kwa nguvu.
Dk. Kassim M.P. Haumotile,
S.L.P. 25578,
Dar es Salaam.
Yataka kutafakari
Lazima kuwa makini, jambo kulifikiria,
Vizuri uketi chini, uwaze umetulia,
Utakijua kiini, upate kinofatia,
Wewe mja kujijua, yataka kutakafari.
Waweza kuwa huoni, ingawa waangalia,
Ziko wazi zako mboni, na jicho umekodoa,
Jiulize nafsini, usende unapamia,
Njia njema kuijua, yataka kutafakari.
Tutakuona khaini, kuacha ya sawa njia,
Yalo mema huyaoni, dalili unafumbia,
Ukijikuta shimoni, uanze kutulilia,
Ya kheri ili kujua, yataka kutafakari.
Kutegemea maoni, na kwako kutamania,
Uishi huku kidhani, umeiumba dunia,
Na khatia Insani, hebu kwa Mola rudia,
Na lengo kuligundua, yataka kutafakari.
Hata kukaa kitini, wenzio watawalia,
Huwajali walo chini, walokuweka raia,
Ni kinyume cha yamini, haufai kubakia,
Shukurani kuijua, yataka kutafakari.
Utu unayo thamani, huupati kwa rupia,
Ni kutenda yenye shani, alofaradhi Jalia,
Wamepita duniani, haya walokiyajua,
Matendo kuyatambua, yataka kutafakari.
Kumjua hayawani, na mtu alotimia,
Hakuhitaji miwani, bali bongo kutumia,
Na aya za kitabuni, hili zimetuambia,
Na ili kuzivumbua, yataka kutakafari.
Kumkiri Rahmaani, mmiliki wa dunia,
Mtengeneza kila fani, uluma na hukumia,
Inahitaji yakini, na nuru kuangazia,
Njia tutoipotea, yataka kutafakari.
Kuwajua mumiani, wabakaji wa sheria,
Waloshika usukani, mbele wakatangulia,
Kundi moja kuthamini, na jingine kubagua,
Na dhuluma kuijua, yataka kutafakari.
Zipo pia za kigeni, siasa tunotumia,
“Demo” ya Kimarekani, na Ulaya “Shamalia”,
Ni utumwa uso fani, sisi tumeuridhia,
Ubayawe kuujua, yataka kutafakari.
Witiri ninasaini, hapa kituo natia,
Ni ibada kwenye dini, kutafakari kadhia,
Ajabu kwa waumini, hili kutozingatia,
Tafsiri ya “Uwazi”, yataka kutafakari.
Jihad R. Saballa,
Box 347,
Shinyanga.
Mkwezi (swali na. 1)
Ninawaomba malenga, popote ulimwenguni,
Mambo yameshanitinga, sijui nifanye nini,
Na roho inanitanga, jawabu nipatieni,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Chanzo cha kisa ni kwamba, nilikuhama mjini,
Nikaenda hamia shamba, huko kwetu minazini,
Nikalununua shamba, la minazi fahamuni,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Nazi zilipokomaa, nilikuwa furahani,
Mkwezi nikachukua, hodari kwa hii fani,
Zana zake akatwaa, akaingia shambani,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Mitiye mirefu sana, inanepa kileleni,
Mkwezi kavaa zana, akapanda mnazini,
Yuwaimba akinena, wakati mimi ni chini,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Katikati akakwama, si juu wala si chini,
Akaanza kulalama, mimi nakufa jamani,
Ninajiachia jama, nguvu zaenda mwishoni,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Mimi sijui kupanda, huko juu mnazini,
Kijijini nako kwenda, ni mbali sana jamani,
Kila ninavyojipinda, la kufanya silioni,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Nabaki najiuliza, huyu ni mkwezi gani,
Pia na kujisemeza, huu ni mnazi gani,
Ni jambo la kushangaza, ushauri natamani,
Mkwezi ameshakwama, walimwengu nifanyeni?
Nasaha ninazitaka, asianguke mtini,
Tena hima kwa haraka, asijedondoka chini,
Mkichelewa hakika, mtaingia lawamani,
Mkwezi ataanguka, walimwengu tufanyeni?
Juma M. Bwanakheri,
S.L.P. 45245,
Dar es Salaam.
Mola muweke peponi (Siraji)
Bismilahi Muumba, ulioumba ulimwengu,
Mimi kwako ninaomba, umsamehe mwanangu,
Machozi yamenikaba, nipo hoi hali yangu,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Juhudi tulionyesha, kikeni na kiumeni,
Madawa tulimwosha, ya ndani na ya kigeni,
Na dua hatukuacha, siku zote midomoni,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Siku ya tarehe tatu, Siraji ametutoka,
Ni siku ya Jumatatu, mwezi wa nane hakika,
Mola akamtunuku, kamwita akaitika,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Siku ya tarehe nne, Siraji tukamzika,
Kwa wake na waume, wote walimiminika,
Ikafanywa shime shime, mwenzetu kwenda kuwekwa,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Iwapo nilitamka, baya kubwa kwa mwanangu,
Na Mola ukaandika, nafuta kauli yangu,
Ila mema nayataka, umjazie mwanangu,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Yarabi takabalia, dua hii kwa mwanangu,
Pazuri muandalia, muondolee machungu,
Peponi kwenda tulia, nakuomba Mola wangu,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Beti hizi naishia, mambo yamenizidia,
Mola ninakuachia, Muweke ulotimia,
Motoni kutofikia, Siraji wangu nalia,
Mola muweke peponi, (Siraji) bin Himidi.
Safina Omar
C/o Fauziya Jabiry Katundu,
Magomeni Kondoa St. No. 16
Dar es Salaam.
Ni basi tumeuawa?
Bismillah Rahmani, Mola unoabudiwa,
Kusudio la imani, Rabi unotegemewa,
Waweke pema peponi, wenzetu walouawa,
Mwembechai Magomeni, ni basi tumeuawa?
Wamekufa watu thani, wenzetu wamelipuliwa,
Damu ilokuwa chini, kwa mchanga kufukiwa,
Ni kama vile kunguni, haki yake kuuawa,
Atatetewa na nani, Ni basi tumeuawa?
Mauaji ya Jijini, yafaa kushutumiwa,
Faraka ziwe pembeni, umoja unatakiwa,
Na tofauti za dini, Kusupa mezitenguwa,
Wote twapenda amani, ni basi tumeuawa?
Mbiu yangu Kigamboni, mpaka huko Lujewa,
Wa Kigoma vijijini, Mbinga, Nzega na Ludwa,
Mafia, Mlingotini, Ngara, Magu, Kaliuwa,
Tunachongojea nini, ni basi tumeuawa?
Rukwa, Mtwara njooni, wenzenu tumeonewa,
Mwembechai Magomeni, wenzetu wameuawa,
Sababu khasa ni nini, muuaji hajatowa,
Tutangoja hadi lini, ni basi tumeuawa?
Hivi ni amani gani, ambayo imetishwa?
Tanga na Ngaramtoni, Morani mnachelewa!
Serikali ihojini, kwani vipi yalikuwa,
Mauaji Magomeni, ni basi tumeuawa?
Iguguno, Turiani, Musoma mnangojewa,
Kwa pamoja tulaani, kwa huku kuhujumiwa,
Tuwahi mahakamani, tume tukishaundiwa,
Tusikae mashakani, ni basi tumeuawa?
Shinyanga, Hale, Bumbwini, na Kanda yote ya Ziwa,
Matipwili, Kibaoni, Mwidu kwa Mfuga Njiwa,
Rombo, Kibororoni, wenzetu wameuawa,
Mchango wenu ni nini, ni basi tumeuawa?
Dodoma kule Bungeni, hili lilishangiliwa,
Kule kusema pigeni, mependa waheshimiwa,
Wizara Mambo ya Ndani, na Bajeti imepewa,
Tulichojifunza ni nini, ni basi tumeuawa?
Kumi ni kaditamani, na ngoja kuitikiwa,
Wote wapenda amani, kwa hamu mnangojewa,
Linze, Nitu mlikoni, mlochoka dhulumiwa,
Serikali ihojini, ni basi tumeuliwa?
Wabilah Tawfiq
K.S. Luanda (Nolo)
Dar es Salaam
|
YALIYOMO
TAHARIRI
HAKI YA KUABUDU MASHULENI: Hoja ya uwingi isizuie haki
ya wachache
Aliyeandika Yesu si Mungu bado akabiliwa
na kesi
Na Mwandishi Wetu
Wazazi walia na Mkuu wa shule
Mkwawa
Na Mwandishi Wetu, Iringa
Serikali iache kudhulumu
Waislamu - Bakwata
Na Mwandishi Wetu,
KESI YA MIRATHI: Hukumu ya
Jaji Agostino yatupwa
Na Mwandishi Wetu
Sumaye sasa atoa ‘waadhi’ Msikitini
Na Mwandishi Wetu, Arusha
Sekondari ya Kiislamu Sumbawanga,
mtihani kwenu – Sheikh Akilimali
Na Harun Rashid, Sumbawanga
37 wasilimu Mwanza
Na Mwandishi Wetu, Mwanza
Akamatwa kwa kusoma gazeti
la ANNUUR !
MGOGORO WA CHWAKA NA MARUMBI: Serikali
ya Dk. Salmin itafute ufumbuzi
Na Mwandishi Wetu, Pemba
MAPENDEKEZO YA KATIBA YA SHIRIKISHO
LA TANZANIA - 4
Kwa nini walengwa wa mabomu wawe ni
Marekani?
Na Maalim Ali Bassaleh
Profesa amekosea kusema kwamba...
Na A.M. Hamza
Ugaidi ni ugaidi, hata wa Marekani
ni ugaidi
Na Maalim Ali Bassaleh
Dhana ya Udugu wa kiislamu
UGAIDI: Chanzo si magaidi, ni dhuluma
ya Marekani
Na HASSAN KIMANGALE
Jengeni familia bora
Na Abuu Said, Iringa
Tuwasaidie Waislamu kielimu
na kiuchumi - Bi Zuhura
Na SAID RAMADHANI KISSIMBA
Tumieni uhuru wenu vyema
Na Abuu Zaina, Iringa
Hoja za kutofautisha Yesu na Issa
ni udhaifu, ni uzushi mtupu! - 4
Na Muhibu Said
Mihadhara ya Wakristo yatawala Handeni
Na Mwandishi Wetu, Handeni
Ziara ya Kadinali Pengo Moro
Na Mussa Ally, Morogoro
Aonyesha ujuzi wa kutengeneza
Trekta
Na Mwandishi Wetu
Waislamu wasizifanye sharia
za dini kuwa nzito – Sheikh Mzonge
Na Ashraf Yusuf, Moshi
Sengerema waomba msaada
Na Idd Katimba, Mwanza
Mafundisho ya Quran
Barua za wasomaji
Mashairi:
Masomo ya dini ya Kiislam
Chakula na Lishe
Matunzo ya mtoto mwenye lishe duni
Matangazo
|