AN-NUUR 
Na.176 Shaaban  1419, Novemba 20 - 26, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Silaha yetu ni kura ya pamoja
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC U.S.A
 
 

KATIKA makala iliyotangulia, nilizungumzia unyonge unaotukuta Waislamu, katika kupuuzwa, kudharauliwa na kunyanyaswa na vyombo vyetu wenyewe vya vyama na serikali nchini mwetu. Pia nikasisitiza umuhimu wa kutafuta kwanza na kushika barabara Ufalme wa kisiasa, ili tuweze kwa uhakika kulinda, kukuza na kuimarisha maslahi yetu bila ya kukiuka maadili ya Uislamu kwa kuwadhalilisha wananchi wenzetu wasiokuwa Waislamu. 

Waislamu tuna bahati nzuri kubwa sana ya kuwa na mwanga (sio mwenge) katika Qur’an na Sunnah. Kama tungezingatia mwanga huu, haya yote yanayotukabili hii leo yasingekuwepo. Tunaambiwa katika Suratul-Al-Imraan, aya ya 103 "Na shikamaneni kwa kamba ya Mwenyezi Mungu nyote, wala msiachane, na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu, mlikuwa maadui, naye akaziunganisha nyoyo zenu, hivyo mkawa ndugu, na mlikuwa ukingoni wa shimo la jahanamu, naye akakukoeni nalo. Nanma hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni aya zake ili mpate kuongoka". 

Tumeagizwa Waislamu kupendana, kuhurumiana, kushirikiana, kulindana, kusaidiana na mengi yaliyo mazuri na mema. Na huo ndio msingi wa kuwa kila Muislamu ni ndugu wa Muislamu mwenzake. Tukihimizana na kuyafuata hayo, kwa haki Lillah, haitakuwa kazi nzito kwetu kuupata ufalme wa kisiasa. 

Waislamu hatuna haja ya chama (kwanza wala hakitaandikishwa na wahusika). Uislamu wenyewe ni chama tosha. Hatuna haja ya kadi (La illah il Allah, Muhammad rasul Allah), inatosha kuwa kadi yetu. Hatuna haja ya michango ya kila mwezi, sadaka zetu zinatosha kuwa michango yetu ya kila siku. Hatuna haja ya nyumba kumi kumi, Misikiti yetu inatosha kuwa matawi yetu. Hatuna haja ya mikutano ya hadhara Jangwani wala kule kidongo chekundu au Mnazi Mmoja (hatutapewa vibali), mikutano yetu mitano ya kila siku na mkutano wetu mkubwa wa kila Ijumaa, tuliyopangiwa na Mwenyezi Mungu (s.w) inatutosha. Hiki si chama, hii ni Dini yetu. Kuitangaza ni wajibu wetu, kuipenda, kuifuata na kuitekeleza ni lazima kwetu. Kupata maslahi ya Waislamu na Uislamu wenyewe ni haki yetu. Hatuiombi wala hatumwombi mtu radhi kuwa na haki hiyo. 

Katika hali hii tuliyonayo leo, ngao yetu ni umoja wetu na silaha yetu ni kura ya pamoja (block vote), katika kila uchaguzi. Iwe ni uchaguzi wa wajumbe wa nyumba kumi kumi, wa kata, wa tawi, wa madiwani, wa taasisi, wa chama, wa wabunge mpaka ule wa Rais. Hatumchagui mtu kwa kuwa ana jina la Kiislamu, la hasha. Lazima tunahikishe kuwa anatuthamini, anatuheshimu, anatulindia maslahi ya Waislamu na Uislamu wenyewe. Waislamu wachangamkie uanachama na uongozi wa vyama vyote vya siasa, tusingojee kupewa, tuchukuwe! Katika hali hiyo, tutaacha kupuuzwa na Insh-Allah, Ufalme wa kisiasa tutautia mikononi mwetu na dhima ya kuomba omba itatutoka. Viongozi wa serikali yetu, waliokalia viti vya dola kwa kura zetu ni watumishi wetu. Sioni sababu ya kwenda kuwaomba, huku mikono yetu iko nyuma, eti watufanyie hiki au kile. Hao tunawatuma tu watufanyie tunayowachagulia watufanyie. Kama wanaonyesha jeuri, basi kazi yetu inakuwa moja tu, kuwatoa katika viti vya dola yetu. 

Kinachohitajika katika kutimiza hayo ni uongozi bora na wafuasi bora walioshiba Uislamu kikweli kweli. Na kuushiba Uislamu ni jukumu na wajibu wa kila mmoja wetu. Hapa panahitajika kumwogopa na kumtii Mwenyezi Mungu (s.a.w) na Mtume wake Muhammad (s.a.w.). Kwa maneno mengine, tunahitajika kupigana jihadi kubwa, kila mmoja wetu na nafsi yake mwenyewe kwanza. 

Viongozi wa Uislamu na wale wa Kiislamu, ili kufanikisha, lazima wajizatiti na kuwa majasiri. Na kuwa pamoja katika malengo yao na uongozi wao. Ni muhimu kwao kuondoa matatizo yao ya kibinafsi ndani ya Misikiti yao na majumba yao kwa faragha, hekima na taadhima. Kinyume cha hayo, watakuwa viongozi bandia wasiokomaa vichwani mwao na hivyo watakuwa wameshindwa kuonyesha sifa za uongozi wa Uislamu na waumini wake. Na wafuasi wa Kiislamu na Uislamu wanatakiwa kuwa na sifa na tabia hizo hizo. 

Katika harakati za kujitafutia Ufalme wa kisiasa, lazima kuna matatizo yatakayojitokeza. Yale tunayoyategemea ni lazima tuyazungumze kabla ya kujitokeza kwake. Linalokuja haraka akili ni lile la Waislamu wasaliti (ndumilakuwili), waoga (watetea matumbo na vyeo vyao), wanafiki (akina popo hao) na wale waliochanganyikiwa (hawajui wayafanyayo). Hao hatuna haja ya kuwapiga pande na kuwasusa. Tuukumbuke mfano wa Sayidna Omar, huenda katika hao pakapatikana askari wazuri wa Uislamu. Chuki, husda, visasi, kukomoana na choyo kamwe havitatusaidia. Tujifunze kuvumiliana, kusameheana, kufundishana na kuaminiana. 

Lipo pia tatizo la huyu Suni, yule Maliki na wale hivi na hao vile. Tujiulize kwanza, Mtume wetu mpendwa alikuwa kundi gani katika makundi hayo? Aliye bora kati yetu ni yule amchae Mwenyezi Mungu (s.w) na hakuna kati yetu anayemjua au anayejijua. Kwa hiyo tusipoteze malengo yetu katika kushughulikia yaliyokuwa juu ya uwezo wetu. Kazi yetu kubwa ni kujiombea nafsi zetu wenyewe na kuombeana kati yetu. Kukosoana ni wajibu, lakini tunawajibika kuwa na hekima na taadhima, siyo kudharauliana, kukebehiana. Itakuwa tunalikataa lipi na tunalifanya lipi. 

Mbali ya hayo na mengine kama hayo, kuna suala la Misikiti. Sheikh au Imamu wa Msikiti huu hasemi na Sheikh wa Msikiti ule. Mimi Msikiti wangu ule, si swali Msikiti huu na yanayofanana na hayo, wallahi, mimi bado sijajua vigezo kama hivi vinatoka wapi. Mambo kama hayo tunahitajika kujihadhari nayo sana, ndiyo yanayochangia kutuletea unyonge huu tulionao hivi sasa. Ili kujikomboa tujiepushe nayo. 

Viongozi wa Misikiti, Madrasa, taasisi na vyombo vingine vya Kiislamu kama vile Baraza Kuu, Tabligh, Warsha, Ansaar kwa mfano, lzima vijishughulishe katika ngazi kuanzia mashina, kata, matawi, wilaya, mikoa na kitaifa. Na katika ngazi zote hizo kuwepo chombo kinachowawakilisha wote katika mfumo wa "United Front" au "Coalition" ya namna moja au nyingine. Kupitia umoja huo, uamuzi ukitamkwa unakuwa wa sauti moja kwa vile kila chombo kina uwakilisho katika hiyo "United Front" au "Coalition" inayohusika. Nadhani sote tunaelewa kuwa Roma haikujengwa siku moja. Hebu tujaribu katika uchaguzi unaokuja mwaka 2000. Tukipata mafanikio hata kidogo tu, kazi yetu inabakia pale pale kutumia akili zetu. Daima mbele, nyuma katu. Tumedhalilishwa vya kutosha, tumetumiwa vya kutosha, lazima sasa tuseme sasa basi. 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
Maoni 
Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha 

Sakata la mabucha  ya Nguruwe kuibuka upya 
Na Mwandishi Wetu  

Kondom sio kinga ya Ukimwi 

Bakwata yairushia polisi makombora Ngaramtoni 

MACHO YA SHUTUMA 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Serikali yatakiwa iwachukulie hatua wauaji 
Na Mwandishi Wetu 

Historia ya Msikiti wa Ngaramtoni 

Silaha yetu ni kura ya pamoja 
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC  U.S.A 

Anuani ya fikra 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Kuukaribisha mwezi mtukufu 

Tunahitaji "UN' ya Waislamu! 
Na Said  Rajab 

Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana 

Umuhimu wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2 
Na Ustaadh Kupa Pazi Said 

Kesi mojawapo ya mihadhara yafutwa 

Wasaidieni watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo 

Mahafali ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao 

Wanafunzi Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa 
Na Iddi M. Katiba, Mwanza 

Saidianeni katika shida - Sheikh Abdallah 

Waislamu, Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja 

Someni  muiokoe jamii kimaadili 

Acheni Shirki 

Kesi nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa 
Na Muhibu Said 

Kusilimu kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza 

Nzasa waomba msaada wa chakula, madawa 

Katibu wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini 

Masomo ya Dini ya Kiislamu  

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Umuhimu wa chakula katika shule za awali]  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita