AN-NUUR 
Na.176 Shaaban  1419, Novemba 20 - 26, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana
 
  • Washiriki walitoka Lindi mjini, Mtwara mjini, Nachingwea, Masasi na Newala
  • Mauaji ya Mwembechai yalaaniwa
  • Waahidi kutorudia makosa mwaka 2000
KONGAMANO lilianza saa mbili asubuhi kwa kupokea maandamano ya akinamama yalioanzia katika pande zote za mji wa Newala. Kuanzia katika misikiti mitano mashuhuri na kumalizikia katika msikiti wa HIDAYA uliopo eneo la NANGAWALA ambapo ndipo lilipofanyika kongamano. Maandamano hayo yalipokelewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kutetea Haki za Akinamama, Bi Fatuma Lazaro. 

Ikufuatia dua ya ufunguzi iliyotolewa na Bi. Halima Mnyamanzi kutoka AL-AZIZ Islamic Centre Masasi. Qur’an ilisomwa na Ukt Halima Nanjocha, kisha Mwenyekiti wa akinamama wa Newala Mama Ndija aliwakaribisha washiriki wote kuwatambulisha wageni. Ilisomwa risala ya akinamama wa Newala iliosomwa na Katibu wao Sharifa Ntangashari. 

Kongamano lilikusanya akinamama kutoka Newala, Lindi, Mtwara, Masasi, Nachingwea, Dodoma, Dar es Salaam na Kilwa. Jumla ya washiriki walikuwa 2800. 

Mada mbalimbali zilitolewa katika mtiririko ufuatao:- 

Mada ya kwanza ilihusu vazi la Hijab - Ilitolewa na Ukht. Fatma Juma ambaye alielezea ulazima wa vazi hili la Kiislamu, na alikemea sana tabia ya kwenda uchi na kuvaa nguo fupi, na akailaumu Serikali kwa kuruhusu mashindano ya kuwa uchi, yanaitwa ya urembo, wakati ni kumkashifu mwanamke. Aliwataka akinamama waliopo maofisini, wizarani, hospitali, michezoni, jeshini, na kwingineko wavae Hijabu wasidhani huko waliko hakuna Mungu. 

Akigusia tukio la Mwembechai alisema Serikali ya CCM iliwauwa akinamama, kuwadhalisha na kuwakashifu, wakati wakiwa msikitini,"huu ni unyama wa wazi, nashangaa kwanini mpaka leo wanaume hawajalipia kisasi, wakati Mtume (s.a.w.) alipigana vita na Mayahudi wa Qainuqaa kwa kumvua mwanake Hijabu", alisema na kuongeza. "Sijui kama kuna wanaume wa kweli hapa Tanzania." Akamalizia kwa kusema umefika wakati "sisi wanawake tuanze kazi." 

Mada ya pili ilikuwa juu ya Nafasi ya Waislamu hapa ulimwenguni. Mada hii ilitolewa na Mwenyekiti wa Idara ya Uhamasishaji wa Kamati ya akinamama Taifa Ukht Arafa. Yeye alizungumzia lengo la kuumbwa mwanadamu na sababu ya kuletwa hapa duniani na lipi wanatakiwa kufanya. 

Alieleza kuwa Muislamu ndio khalifa na ndio kiongozi wa Ulimwengu na ndio mwenye kuimarisha haki na usawa. 

Alisisitiza kuwa makafiri wao ni waharibifu na lengo lao ni kustarehe na kula. Hata siku moja hawapo tayari kupata matatizo bali hufanya juhudi za makusudi kuwatia wenzao matatizoni. Umefika wakati alisema Waislamu washike nafasi yao ya kuongoza dunia. 

Alisisitiza kuwa Uislamu ni mfumo kamili wa maisha, popote pale alipo Muislamu anatakiwa autekeleze Uislamu wake, iwe ni ofisini, nyumbani, shambani, Bungeni, vitani, michezoni n.k. 

Alimaliza mada yake kwa kuwataka Waislamu wote wake kwa waume wahamasishane juu ya kurejesha hadhi yao na kuchukua nafasi yao na kwamba Qur’an ndio katiba yao na umefika wakati sasa Waislamu waanzishe chama cha siasa chenye misingi ya Kiislamu na waanze kufanya kampeni. 

Mada ya tatu ilikuwa juu ya tukio la Mwembe Chai. Mada hii ilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Akinamama Taifa, Bi Fatma Lazaro. Alielezea chanzo na asili ya tukio la Mwembechai toka kauli ya Rais kule Tabora. Alisisitiza kwamba Waislamu wanaidai Serikali iunde tume huru ya uchunguzi, walioua wafikishwe mahakamani na wote waliodhalilisha wanawake wachukuliwe hatua za kisheria. Akinamama wengi walitokwa na machozi baada ya kusikia tukio la Mwembe Chai. 

Akazungumzia hali ya miji ya Waislamu. 

Alisema barabara kuu ya Dar es Salaam hadi Liwale ni mbovu sana haipitiki kabisa kuanzia Mnazi Mmoja mpaka Mtwara barabara ni mbovu kabisa haipitiki kwanini maeneo ya Waislamu barabara ni mbovu", alihoji. 

Kongamano liliendelea mpaka saa kumi na moja na nusu kwa maonyesho mbalimbali ya Hijabu na mengineyo. 

Hatimae kutoa maoni na maazimio yafuatayao:- 

1. Kufanya kongamano kubwa sana la Kanda ya Kusini mwakani 1999. 

2. Kutokurudia makosa mwaka 2000. 

3. Kudumisha umoja na mshikamano na kuunda Jumuia ya akinamama wa Kanda ya Kusini. 

4. Kulaani mauaji ya Mwembechai, kuitaka Serikali iwafikishe mahakamani wahusika. 

5. Kuanzisha darsa za akinamama kila msikiti. 

6. Kufanya mikutano ya Kiwilaya na Kimkoa kila mwezi. 

7. Kila msikiti/madrasa uanzishe chekechea. 

8.. Waislamu wafanye sensa kila msikiti wajuane. 

Baada ya kongamano kumalizika, Ustadh Yusuf Kayungilo alizungumza kwa niaba ya wazee na Waislamu wa Newala, na wakaahidi kuwaunga mkono akinamama kwa hali na mali. 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
Maoni 
Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha 

Sakata la mabucha  ya Nguruwe kuibuka upya 
Na Mwandishi Wetu  

Kondom sio kinga ya Ukimwi 

Bakwata yairushia polisi makombora Ngaramtoni 

MACHO YA SHUTUMA 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Serikali yatakiwa iwachukulie hatua wauaji 
Na Mwandishi Wetu 

Historia ya Msikiti wa Ngaramtoni 

Silaha yetu ni kura ya pamoja 
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC  U.S.A 

Anuani ya fikra 
Na Abu Halima Sa Changwa 

Kuukaribisha mwezi mtukufu 

Tunahitaji "UN' ya Waislamu! 
Na Said  Rajab 

Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana 

Umuhimu wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2 
Na Ustaadh Kupa Pazi Said 

Kesi mojawapo ya mihadhara yafutwa 

Wasaidieni watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo 

Mahafali ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao 

Wanafunzi Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa 
Na Iddi M. Katiba, Mwanza 

Saidianeni katika shida - Sheikh Abdallah 

Waislamu, Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja 

Someni  muiokoe jamii kimaadili 

Acheni Shirki 

Kesi nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa 
Na Muhibu Said 

Kusilimu kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza 

Nzasa waomba msaada wa chakula, madawa 

Katibu wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini 

Masomo ya Dini ya Kiislamu  

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Umuhimu wa chakula katika shule za awali]  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita