|
|
|
Yatupasa tujishangae nini kimetusibu Walimwengu wa leo. Iweje pamoja na akili zetu tuaminizo kuwa timamu tudhanie kwamba mtu akiwa hana mali au maguvu hana akili. Kwamba yeye hathubutu japo kusimama na kusema jambo fulani halifai, maadhali mkubwa kasema! Inashangaza na kusikitisha bali na kutia huzuni kwamba watu wote kuanzia viongozi wa nchi, vyombo vya habari na taasisi mbali mbali duniani wamesita kufikiri kwa akili zao ila hunena na kufikiri kwa akili za wengine. Wamegeuka kuwa vipaza sauti na wacheza ngoma inayopigiwa kwingine. Ulimwengu mzima hivi sasa unacheza zumari inayopigwa na Marekani kwamba Saddam Hussein lazima ashirikiane na wakaguzi wa silaha wa Umoja wa Mataifa la sivyo ataadhibiwa kijeshi. Hakuna hata mmoja anayehoji kwamba je hilo linaloitwa azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lina uhalali gani? Pili je ni Iraq pekee iliyo na silaha zinazohitaji ukaguzi na kuangamizwa? Tatu Marekani ina uso gani kimaadili na uwajibikaji wa kusimamia, utengamano na amani ya mataifa mbalimbali duniani. Kinachojitokeza hapa ni kwamba Marekani kwa ubabe wake sio tu kwamba inaziburuza nchi nyingine pamoja na vyombo vinavyoitwa vya kimataifa, lakini hufanya itakavyo kwa kujua hakuna yeyote wa kuidhibiti. Maguvu yamefanywa ndio haki na hivyo kuifanya dunia itawaliwe na ubabe wa Marekani. Zipo nchi kama Uingereza ambazo huitwa Marafiki wa Marekani ambazo kila lisemwalo huko Washington wao ni hewala bwana. Hakika ya mambo hawa si marafiki wala washirika wa Marekani bali ni wanyonge wa Marekani. Uingereza haina inaloweza kupinga dhidi ya Marekani. Katika suala la Iraq Marekani inakuruza kila nchi na chombo cha Umoja wa Mataifa. Lakini Marekani nayo inakuruzwa na sera za Israel. Israel yenyewe ambayo, ina silaha za "Nuklia’ na imekataa kutia saini mkataba wa kuzuia silaha kali za maangamizi na pia ipo Mashariki ya Kati kama Iraq inayoshutumiwa kutishia nchi nyingine za eneo hilo. Marekani imeweka utaratibu ambao kwa vyovyote Iraq itakavyofanya haiwezi kutosheleza madai ya kinachoitwa maazimio ya Baraza la Usalama. Na ndio maana tunasema Iraq ina haki ya kulalamika kwamba haitendewi haki. Marekani yenyewe ina silaha za kila aina pamoja na zile za maangamizi. Hizo zinazoitwa silaha za kemikali (chemical weapons). Mwanzilishi si Iraq. Iraq imenunua kwa hao leo wanaowashutumu. Ipo hoja kwamba tahadhari inachukuliwa ati silaha za hatari zisiangukie mikono ya mtu asiye faa. Je, zikiwa mikononi mwa Marekani ndio zipo kwenye nchi inayofaa? Marekani ambayo imezivamia nchi nyingi na kuleta fujo iliyoleta hasara kubwa ya roho za watu na mali? Na juzi hapa ikaipiga Sudan kwa dhulma na kuzuia Umoja wa Mataifa usifanye uchunguzi! Sasa iweje pamoja na kwamba watu wana akili zao na nchi zinadai huru na zenye demokrasia lakini zinashindwa japo kusema. Zamani wakati wa TANU kulikuwa na msemo "Mawazo ya kufugwa". Sasa leo kama mtu hushindwa kuyapima mambo na kuamua kwa akili yake si ni utumwa ule ule. Yawezekana Serikali na nchi mbalimbali tukiwemo Tanzania, zimenyamaza kwasababu ni kaa la moto mguuni mwa wenzako. Ni Iraq itakayopigwa. Lakini kesho waweza kutushinikiza na masera yao bila kujali wananchi wetu wataathirika vipi na itatubidi tusalimu amri. Hapo ile dhana ya Taifa huru itakuwa imepoteza maana yake. |
YALIYOMO
Maoni Kuwa na mawazo ya kufugwa tunajidharaulisha Sakata la
mabucha ya Nguruwe kuibuka upya
Bakwata yairushia polisi makombora Ngaramtoni MACHO YA
SHUTUMA
Serikali
yatakiwa iwachukulie hatua wauaji
Historia ya Msikiti wa Ngaramtoni Silaha yetu
ni kura ya pamoja
Anuani
ya fikra
Tunahitaji
"UN' ya Waislamu!
Kongamano la wanawake wa Kiislamu Newala lafana Umuhimu
wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo - 2
Kesi mojawapo ya mihadhara yafutwa Wasaidieni watoto wenye vipaji - Prof. Kilonzo Mahafali ya kidato cha nne Thaqafa: Wazazi wakumbushwa wajibu wao Wanafunzi
Mwanza wadai haki za kuabudu mashuleni kwa usawa
Saidianeni katika shida - Sheikh Abdallah Waislamu, Wakristo Rufiji watakiwa kuunda umoja Someni muiokoe jamii kimaadili Kesi
nyingine ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa
Kusilimu kwa Wakristo kwaleta kero Mwanza Nzasa waomba msaada wa chakula, madawa Katibu wa Bakwata Moro ang'olewa Msikitini Chakula
na lishe
|