AN-NUUR  
Na.175 Rajab 1419, Novemba 13 - 19, 1998 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Katibu wa Baraza Kuu azikwa Dar
 
  • Ni Sheikh Abas Kilima
  • Alifariki dunia na mkewe katika ajali ya gari Chalinze
  • Maelfu wahudhuria mazishi yake
Na Mwandishi Wetu

WIKI moja baada ya kuikumbusha serikali ijiunge na Shirika la OIC, Katibu wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Abas Kilima amefariki dunia katika ajali ya gari alfajiri ya Jumamosi Novemba 7, mwaka huu. 

Kwa mujibu wa mdogo wa marehemu, Bw. Ali Kilima, ajali hiyo ilitokea Chalinze mkoa wa Pwani ambako marehemu alikuwa njiani kurejea Jijini akitokea Kondoa kuhudhuria mazishi ya mwanawe aliyefariki dunia mwanzoni mwa wiki iliyopita. 

Katika ajali hiyo, mke wa marehemu Bi. Rukia Fundi pia alifariki dunia papo hapo. 

Akisimulia jinsi ajali hiyo ilivyotokea, Bw. Ali Kilima alisema gari walilokuwa wakisafiria lilianza kuyumba kabla ya kupinduka mara kadhaa na kusababisha vifo hivyo. 

Katika gari hilo walikuwemo pia ndugu, mtoto na mjukuu wa marehemu pamoja na dereva ambao walisalimika bila kupata majeraha yeyote. 

Marehemu wote wawili walizikwa siku ya Jumapili Novemba 8, 1998 katika makaburi ya Kisutu katikati ya Jiji. 

Siku chache kabla ya safari yake Alhamisi jioni, Sheikh Abas Kilima aliandaa kongamano lililowakusanya Waislamu kutoka sehemu mbalimbali nchini. 

Kongamano hilo lililofanyika Novemba 1, mwaka huu Temeke Jijini Dar es Salaam, lilizungumzia pamoja na mambo mengine hali ya Waislamu nchini na uadui ulio dhidi yao katika nyanja mbalimbali. 

Wakati akiwasilisha taarifa ya Baraza Kuu katika kongamano hilo, marehemu Sheikh Abas Kilima aliikumbusha serikali kutimiza ahadi iliyotoa ya kujiunga na Shirika la OIC. 

Alieleza kunyong’onyea kwa nchi kiuchumi kwamba ni mojawapo ya sababu zilizolifanya baraza lake kuikumbusha serikali ahadi yake iliyotoa. 

Aliwaondoa wasiwasi wale wenye madai kwamba OIC ina malengo ya kuwasilimisha wasio Waislamu, kwa kuwaeleza kwamba ingawa shirika hilo ni la kidini (Islamic Organization) lakini malengo yake ni kuboresha hali za kijamii za nchi wanachama wake kwa kuzipa misaada na mikopo isiyo na riba. 

Wakati huo huo, maelfu ya waumini wa dini ya Kiislamu Jijini Dar es Salaam walishiriki mazishi ya marehemu Abasi Kilima na mkewe. 

Kuanzia nyumbani kwa marehemu Kijitonyama, waumini hao walifurika jioni ya Jumamosi hadi majeneza yanaondoka mahala hapo kuelekea Msikiti wa Tanzania Islamic Centre Magomeni kulikotolewa nasaha mbalimbali kabla ya swala ya Jeneza. 

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia umati wa waumini ukifunga barabara ya Morogoro na kusababisha magari yaliyotokea Ubungo na Mwenge na yale ya Kariakoo kusimama kwa masaa kadhaa wakati majeneza yakisindikizwa kuelekea makaburi ya Kisutu. 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
Maoni  
Kuvuja kwa mitihani: Tuweni wakweli kwa nchi yetu  

Katibu wa Baraza Kuu  azikwa Dar  
Na Mwandishi Wetu  

Ubabe wa madhalimu kuzimwa:  
Na Mwandishi Wetu  

MACHO YA SHUTUMA  
Na Abu Halima Sa Changwa  

Wazo mpachiko (Programmed mind)  
Na Abu Halima Sa Changwa  

Ta'azia: Abbas Shaaban Kilima 1938-1998  

Wasemavyo Wanaharakati  

Mdahalo kati ya Waislamu na Wakristo- 4  
Na Nandenga wa Mkomidachi  

Siri ya Miujiza  
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa  

Umuhimu wa Elimu ya Awali kwa watoto wadogo  
Na Ustaadh Kupa Pazi Said  

Ifahamu Madrasat Ghazal Muslim - Moro  
Na Mussa Ally, Morogoro  

Pamoja na sala, tusimamishe zakah  
Na Abubakari S. Marwillo  

Aina za maudhi yaliyoharamishwa juu ya Muislamu  
Na. Ramla  

Israi na Miiraji ni miujiza  
Mwandishi: Maalim Bassaleh  

Pamoja na ahadi ya Serikali kuzifuta: kesi za mihadhara zaendelea mahakamani  
Na Muhibu Said  

Waislamu Uluguruni  Moro wazama kwenye matambiko  

Imarisheni miradi ya elimu -  Prof.  Mikidadi  
Na Mwandishi Wetu, Dodoma  

Teknologia: Jifunze Kuunganisha Kompyuta (5)  
Na Hassan Omar  

Mafunzo ya Qur'an  
Shetani anawaogopesha wenye mali kutoa  

Chakula na lishe  
[Kansa ya tumbo]  

Matangazo  
 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita