AN-NUUR 
Na.178 Shaaban  1419, Desemba 4 - 10, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Someni kwa ajili ya Allah - Sheikh Baruti
 

Na Muhibu Said 

MKURUGENZI wa shirika la kiislamu la kutoa misaada la Islamic African Relief Agency (I.A.R.A.) nchini, Sheikh Idrisa Omari Baruti, amewakumbusha Waislamu wajibu wao wa kuitafuta elimu oyote popote bila kubagua. 

Aidha Sheikh Baruti amewatahadharisha Waislamu kwamba daima watakuwa ni wenye kupata hasara kwa ibada zao kwa kuambulia patupu iwapo wataendelea kuzifanya ibada hizo bila Ikhlas (kwa ajili ya Allah S.W.T.). 

Sheikh Baruti aliyasema hayo Jumapili ya Novemba 29, mwaka huu, akiwa mgeni rasmi katika mahafali ya kuhitimisha mwaka wa tano wa kozi ya kuandaa vijana wa madrasa ya IEC Centre, kuingia katika shule za Sekondari (Orientation Kozi). 

Mahfali hiyo iliyofanyika katika msikiti wa Shadhily, Jijini Dar es Salaam, iliandaliwa na taasisi maarufu ya Kiislamu ya Jijini ya Islmic Education Centre (IEC Centre) ambayo ndiyo inayoendesha kozi hiyo. 

Sheikh Baruti alisema jambo la kutafuta elimukwa muislamu limekuwa ni wajibu kwake na kamwe halina mipaka kwani ujumbe wa kwanza alioshushiwa Mtume wetu Muhammad (s.a.w.) ulikuwa ni "kusoma". 

Akifafanua nukta hiyo, Sheikh Baruti alisema ili kuleta ufanisi mzuri katika shughuli zetu za halali za kila siku, Allah (s.w.t.) bado anazo sababu za msingi za kuifanya elimu kuwa ni "amri" kwetu hasa kwa vile imekwishatukirimu vipawa mbali mbali. 

"Kwa hiyo ndugu zangu, tujifunze kwa ajili ya Allah, kwa ajili ya kumtumikia yeye. Na kama hatukumnuia Allah katika ibada zetu, basi tujue kuwa hatupati kitu. Vile vile tusome kwa ajili ya kujenga akhera", alisema Sheikh Baruti. 

Pamoja na maonyesho mbali mbali, ikiwemo Tamthilia iliyobeba ujumbe wa kumcha Allah (s.w.t.) popote ulipo iliyoigizwa na vijana wa madrasa hiyo, pia pamoja na risala ya wanafunzi hao iliyosomwa na mabinti wa madrasa hiyo, kilele cha mahfali hiyo kilihitimishwa kwa baadhi ya washiriki, akiwemo mgeni ramsi wa mahfali hiyo, Sheikh Idrisa O. Baruti, gazeti la AN-NUUR na vijana wanaharakati wa Kiislamu wa Jijini Dar es Salaam kutunukiwa na taasisi hiyo shahada za uhusiano mwema kati yao na taasisi hiyo. 

Shahada nyingine zinazothibitisha tabia njema ikiwa ni pamoja na kutimiza mavazi ya heshima na stara ya Kiislamu ndani na nje ya madrasa, zilitolewa kwa baadhi ya wanafunzi wa madrasa hiyo. 

Aidha zawadi nyingine mbalimbali zilitolewa kwa baadhi ya wanafunzi wa madrasa hiyo wenye sifa za usomaji mzuri wa Qur-an Tukufu, Hadithi sahihi za Mtume (S.A.W.) na wenye mwenendo mzuri na tabia njema madrasani hapo. 

Zawadi hizo pia zilitolewa kwa wanafunzi wenye ushirikiano mwema na waliofanya vizuri katika masomo. 

Taasisi ya IEC Centre yenye makao yake makuu, Mtaa wa Udoe No. 24, Kariakoo, Dar es Salaam, kupitia madrasa yake hiyo yenye mfumo wa kisasa, pamoja na mambo mengine ina programu ya kuendesha kozi mbali mbali, ikiwemo Kiingereza, elimu ya Kiislamu na kadhalika, kwa ajili ya kuwaandaa vijana kuingia katika shule za Sekondari, na kwa watu wazima na wengine wasiojua kusoma kabisa. 

Mafanikio ya madrasa hiyo tangu kuasisiwa kwake ni kuwa kwa asilimia zaidi ya tisini 90% imekuwa ikiwawezesha wanafunzi wake kufaulu vizuri katika shule za Sekondari wanazoingia baada ya kupikwa vizuri na kozi yake. 


Madrasa Al-Ii’Tiswamu Al-Umaahaati Fiisabiililillah - Moro
 

• Ni ushirikiano wa kina mama wa Kiislamu 

• Ilitokana na changamoto ya BALUKTA 
 

Na Rajab Rajab, Morogoro 

MADRASA hii ya ushirikiano wa kina mama wa Kiislamu ipo katika Msikiti maarufu mjini hapa wa Uwanja wa Ndege, ambapo ilianzishwa kutokana na changamoto ya iliyokuwa BALUKTA upande wa kina mama chini ya Mwenyekiti wake Mama Mwanaidi Bashiri na Katibu wake Mariam Amir Mponda. 

Historia ya madrasa hiyo inaanzia mwaka 1988 ambapo ilianza kwa kuwa na wanafunzi kina mama thelathini (30) hadi sasa hivi ina jumla ya wanafunzi 40 na inasimamiwa na walimu watatu ambao ni Mariam Mponda , Mwanaidi Nasibu Jaka na Aisha Juma. 

Aidha, madrasa hiyo katika jitihada zake za kuwapatia elimu kina mama wa Kiislamu wa Morogoro, imeanza kufungua matawi mengine katika Msikiti wa Mafiga (B) ambapo kuna jumla ya wanafunzi 30, madrasa nyingine imefunguliwa Vibandani pamoja na Msikiti wa Nurain uliopo eneo la MUDECO. 

Katika kuhakikisha kuwa wanajiendeleza kiujuzi na kiuchumi, madrasa hiyo ya Al-Iitiswamu wana mpango wa kuanzisha darasa la ushonaji nguo kwa kutumia mashine za cherehani, lakini hata hivyo mpango huo bado unalega lega kutokana na upungufu wa fedha na vifaa mbalimbali. 

Vile vile madrasa hiyo inajishughulisha kwa undani zaidi na utoaji wa Da’awah kwa kutoa mihadhara kwa kina mama ndani na nje ya mji huu hususani vijijini ambapo wanawake wengi wamekuwa nyuma kuhusu elimu ya dini yao na kukosekana madrasa na walimu wa kuwafikishia ujumbe na kuwasomesha. 

Madrasa hiyo ambayo inapokea wasichana wenye umri wa kuanzia miaka 15, inafundisha masomo mbalimbali kama vile Fiqh, Qur’an, Maarifa ya Uislamu, Hadith pamoja na Lugha. 

Akitaja matatizo yanayoikabili madrasa hiyo, Mwalimu Mariam Amir Mponda ameyataja kuwa ni pamoja na upungufu wa vitabu, na wanaume wengi kuwawekea vikwazo wake zao hali ambayo inafanya mahudhurio ya baadhi ya wanafunzi kuwa ya kutoridhisha na kulazimika walimu kurudia rudia masomo yaliyokwisha fundisha. 

Pia Bi. Mariam amewataja watu waliochangia kwa kiasi kikubwa katika kuanzisha na kuendeleza madrasa hiyo ambao amemtaja mama Mwanaidi Muhenga, Sheikh Ayubu Muinge pamoja na Ustadh Suleiman Saddy. 

"Ninatoa wito kwa kina mama wa Kiislamu kuwa suala la kupigania Uislamu siyo la kina baba peke yao, bali kina mama nao wana wajibu mkubwa katika kupigania dini yao kwa hali na mali pamoja na kuipa elimu kipaumbele", alimalizia Bi. Mariam Mponda. 


Madrasat Hidayat Mbagala

Na Mussa Salum 

Miongoni mwa madrasa zilizopata kuwa na kipaji cha kutoa watoto wenye uwezo wa kukariri aya na sura mbalimbali kutoka kwenye kitabu kitukufu chaQur’an na vitabu vingine vya hadithi ni madrasat Hidayat ya Mbagala Kibonde maji Jijini. 

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Mbagala hivi karibuni, mwalimu mkuu msaidizi wa Madrasat hiyo Omari Sultan Mtuliya alisema kuwa Madrasat Hidayat ilianzishwa miaka 13 iliyopita ikiwa na wanafunzi 170 lakini idadi hiyo imekuwa ikishuka kila mwaka kutokana na matatizo kadhaa wa kadhaa ambayo yamekuwa yakiikabili Madrasat hiyo. 

Aliyataja matazo hayo kuwa ni upungufu wa vitabu vya kufundishia kama vile juzuu, misahafu, ubovu wa madrasa ambayo inavuja wakati wa masika na hivyo kuhathiri usomesaji wa watoto katika shule hiyo. 

Matatizo mengine darasa kutokuwa na milango wala madirisha hali ambayo imechangiwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa fedha za kufanyia ukarabati. 

Mwalimu Mtuliya alisema kuwa matatizo ya fedha ambayo yanaikabili madrasat yake yamesababisha mwaka huu kutofanya maulidi ya kupima vipaji vya wanafunzi wa madrasat yake hali iliyomfanya aombe kwa wafadhili mbalimbali ili waisaidie madrasat hiyo kuendesha maulidi hiyo ambayo ilikuwa inafanyika kila mwaka. 

Mwalimu huyo alisema kuwa kwa sasa shule yake ina wanafunzi 120 ambapo idadi ya wavulana na wasichana ni sawa na hupokea wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali za mikoa ya Pwani na Dar es Salaam hasa katika wilaya za Mkuranga, Kisarawe, Rufiji na Temeke. 

Alizitaja mbinu mbalimbali anazotumia kufundishia Mwalimu Omari alisema kuwa anatumia kuwaandikia ubaoni halafu humsimamisha mwanafunzi mmoja mmoja kusoma mara baada ya kumaliza kukariri yale aliyosoma hapo awali. 

Alisema mbinu hii humfanya mwanafunzi kuyaweka yale aliyofundishwa kichwani mwake kwa muda mrefu hali iliyokifanya chuo chake kupata sifa kemkem kutoka kwa wazazi wa wanafunzi wake, shule hiyo hufundishwa na walimu watatu Omari Sultan Mtuliya, Omari Kassimu Mbembeni na Hassan Lyoto. 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
'White Paper  ni ulaghai wa  Serikali ya CCM' 
Na Mwandishi wetu 

Sheikh Omar Bashir awekwa rumande 
Na Mwandishi Wetu 

Mpango wa 'Kupindua' uongozi wa  Bakwata: Masheikh Dar waitwa polisi kuhojiwa 
Na Mwandishi Wetu 

Zahrau Day yatikisa Tanga 
Na Mwandishi Wetu 

MAKALA: Hatuna haja ya maelekezo ya yule aliyetufikisha hapa  
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC USA 

Huduma za afya Kondoa haziridhishi 
Na Abu Zubeir 

Wasemavyo wanaharakati 

Tunahitaji 'UN' ya Waislamu! 
Na Twahir Rashid 

Hoja binafsi: Wawekezaji watuondokesha makwetu 

Jamii inapokuwa soko huria...  
Na Said Rajab 

Someni kwa ajili ya Allah - Sheikh Baruti  
Na Muhibu Said 

Madrasa Al-Ii'Tiswamu Al-Umaahaati Fiisabiililillah - Moro 
Na Rajab Rajab, Morogoro 

Madrasat Hidayat Mbagala 
Na Mussa Salum  

Hali ya Uislamu Moro Vijijini yazidi kuwa mbaya  
Na Rajab Rajab, Morogoro 

Sheikh Masoud Mwinyi awaonya Waislamu kuacha migogoro Babati  
Na Abu Zuberi - Babati 

Tusikaribishe mfungo wa Ramadhani kwa Vunja Jungu  
Na Abeid Poyo 

'Acheni zinaa muepukane na ukimwi'  
Na Mussa Salum 

Wavunja jungu watahadharishwa 
Na Mwandishi Wetu, Morogoro 

Hoja/Uchambuzi: 
Je, hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? 
Na Mwinjilisti Bunga E. Dettu 

Njia ya uzimani ni nyembamba,  waionao ni wachache 
Na Yasin Valerian Massawe 

Habari: 
Semina ya Maimamu Tanga yadai: Maimamu wanapuuzwa  
Na Mwandishi Wetu 

Kesi ya Waislamu Mwembechai yaahirishwa kwa mara nyingine  
Na Muhibu Saidi 

Kongomano la wanawake wa Kiislamu Bagamoyo 
Na Mwandishi Wetu 

Sayansi na Teknolojia 
[Kuongeza RAM kwenye Kompyuta] 
 
Masomo ya Dini ya Kiislamu 

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Madini ya Zinc] 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita