|
|
| Historia
ya mgogoro wa Nzasa
TOKA Msitu wa Kazimzumbwi ufanywe Hifadhi ya Taifa hapakuwahi kutokea mgogoro baina ya Idara ya Misitu na wananchi wa Nzasa wanaoishi kusini mwa msitu huo. Wakati wa operesheni Vijiji ya Ujamaa wananchi wengi walilazimika kuyaacha mashamba yao na kuhamia vijijini. Baadae walirejea kwenye makazi yao ya awali kwenye mashamba yao. Mgogoro ulianza mwaka 1992 walipojiwa na aliyekuwa Afisa Misitu Mkoa wa Pwani, Bw. Beda Kessy na kuambiwa kwamba wanalima katika Msitu wa Taifa. Kwa mujibu wa barua ya wananchi wa Nzasa ya Septemba 5, 1994 kwa Waziri wa Mambo ya Ndani Bw. Kessy alifika kitongojini Nzasa Septemba 13, 1993 akiwa na barua toka kwa Mkuu wa Wilaya inayomruhusu kuweka mipaka ya misitu, kazi ambayo aliifanya. Kuanzia hapo ndipo likaanza shinikizo la kuwataka wahame na wananchi hao wakawa wanapinga wakidai kwamba hawapo katika Hifadhi ya Taifa. Kumbukumbu za kikao cha Februari 19, 1993 kati ya Bw. Kessy na Wana-Nzasa zinaeleza kwamba Bw. Kessy alikuwa amekwenda na ramani ya mwaka 1971 iliyochorwa kwa mkono ambayo hata hivyo ilionyesha kwamba Nzasa ipo Mkoa wa Dar es Salaam na wala si sehemu ya Mkoa wa Pwani wala sehemu ya Msitu wa Kazimzumbwe. Kumbukumbu hizo ambazo zimewekwa sahihi za Mwenyekiti na Katibu wake wa kikao zimeeleza kwamba Bw. Kessy alikiri kwamba Nzasa si sehemu ya msitu, na akaahidi kuandika barua Polisi kufuta kesi aliyokuwa amemfungulia Bw. Mohamed Mtimkavu. Kupitia barua Kumb. Na. MD/F.40/1/28 ya April 21, 1994 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Dar es Salaam iliiandikia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo Mijini kuhusu suala hilo. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ilipendekeza kwamba ili ufumbuzi sahihi upatikane; ni lazima izingatiwe kwamba. Mipaka mipya inayowatia watu wa Nzasa ndani ya Hifadhi ya Msitu iliwekwa na Bw. Kessy mwaka 1993 akiwa Afisa Maliasili Mkoa wa Pwani wakati wananchi hao wapo hapo toka miaka ya 1950. Pili, wananchi hao wana mazao yao ya kudumu, nyumba za kuishi na miradi mbalimbali. Tatu kama ni kuhamishwa itabidi wananchi hao walipwe fidia ya mazao na mali zao. Na pia watafutiwe ardhi nyingine ya kuhamia. Suala hilo lilifikishwa kwa Mhe. Eduward Lowassa akiwa Waziri wa Ardhi, Mei 18, 1994. Mhe. Lowassa alirudisha suala hili kwa Mhe. Ditopile Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam akitoa hoja kwamba suala la misitu lipo nje ya Mamlaka ya Wizara yake na wakati huo kesi ilishafunguliwa mahakamani Bw. Mohamed Mtimkavu alishitakiwa na kupigwa faini ya sh.30,000/- na mahakama ya Kisarawe kwa madai kwamba analima katika eneo la msitu. Aidha Bw. Mtimkavu aliamriwa ahame eneo hilo. Mtimkavu alilipa faini lakini akakata rufaa Mahakama Kuu Dar es Salaam.Katika kesi hiyo No. 149 ya 1994 Jaji W.J. Maina katika hukumu yake alitengua hukumu ya awali kwa kuzingatia hoja mbili. Kwanza sheria ya misitu Cap. 389 Kf. 6(1) inaagiza kwamba kabla ya eneo lolote kufanywa sehemu ya Msitu; ni lazima Waziri atoe tangazo kwa siku 90 likielezea mipaka ya eneo hilo na tangazo lichapishwe katika Gazeti la Serikali.Katika shauri hili hapakuwa na ushahidi wowote wa kuonyesha kwamba hatua hizo zilifuatwa. Pili, kifungu No. 6(1) (c) cha sheria hiyo hiyo ya Misitu kinaagiza kwamba waathirika walipwe fidia, jambo ambalo halikufanyika. Aliyesimama kwa upande wa Misitu wakati huo alikuwa Bw. Charles Secha. Pamoja na hayo mgogoro uliendelea kwa wananchi kughasiwa mara kwa mara. Oktoba 17, 1996 Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam Capt. T.J. Kasapira akimwandikia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Brg. Gen. H. Ngwilizi alimtahadharisha kwamba mgogoro wa Nzasa unatishia kulipua janga kubwa kwa wakazi wa eneo hilo na kwamba wananchi walishaanza kupoteza imani kwa Chama Tawala na Serikali yake. Capt. Kasapira aliomba chama kifahamishwe nini kiini cha tatizo na ni hatua zipi zinachukuliwa na Serikali. Wakati huo wananchi hao walifikisha malalamiko yao kwa Jaji Mkuu; Kitengo cha Sheria na Haki za Binadamu pamoja na Kitengo cha Msaada wa Sheria Kitivo cha Sheria Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Wakati wananchi hao wanahangaika kupata msaada huo wa kisheria ikatoka ilani ya Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe kuwataka wahame. Ilani hiyo ilitolewa Agosti 1, ikitanguliwa na matamko kadhaa ya viongozi wa Serikali akiwemo Makamu wa Rais Mhe. Dk. Omar Ali Juma. Kilichofuatia baada ya hapo ni nyuma
zao kuchomwa moto.
|
YALIYOMO
TAHARIRI Serikali iwahurumie wananchi wake KUCHOMWA MOTO NYUMBA ZA WANANCHI:
Nzasa wamtaka Mkapa awaonyeshe pa kwenda
Mishikaki ya nguruwe Moshi yachomwa
mbele ya Msikiti
MAONI YETU:
Upimaji huu mpya ni wa nini
TANGAZO LA HIFADHI YA MSITU WA KAZIMZUMBWI Ndoa si lengo, ni wasila wa kufikia
lengo
Makala:
Goda Muslim School, Manzese
Utabiri sahihi wa kuibuka kwa Uislamu
Historia ya mgogoro wa Nzasa
DUMT watoa msaada kwa walioathirika
Nzasa
UCHOMAJI NYUMBA NZASA: Wafadhili
wana mchango gani?
Mafundisho ya Quran
|