|
|
|
Kusoma Khitma sh. 5000 Wacheza disko badala ya Maulid Na Mwandishi Wetu BAKWATA wilayani Same imepandisha gharama za huduma zake inazotoa kwa waumini katika kile kinachoonekana kama juhudi za kukabiliana na hali ngumu ya maisha. Kwa mujibu wa taarifa ya Sheikh wa Wilaya, Sheikh Mustafa Mohammed kwa waumini, gharama za kusomewa Khitma na Maulid zimepanda kutoka shilingi 1000 na kuwa shilingi 5000. Aidha, huduma ya kusomewa ‘tatu’ baada ya mazishi itakuwa shilingi 5000 vile vile. Sheikh Mustafa akiongea katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa mjini Same, alisema kuwa huduma ya kufungiwa ndoa itakuwa shilingi 5000 (hizi ni mbali na cheti cha ndoa cha serikali). Hatua hii ya ofisi ya Bakwata kupandisha gharama ya huduma hizi muhimu kwa jamii zimelalamikiwa na waumini wengi mjini hapa hasa ikizingatiwa hali halisi ya kipato cha wananchi. Wengi wamekuwa wakikejeli ongezeko hilo kwa kuliita ‘VAT’ na kusema heri ya ‘VAT’ ya serikali ambayo ni 20% wakati ya Bakwata ni asilimia mia nne (400%). Uchunguzi wa gazeti hili umeonyesha kwamba tayari athari zimeshaanzakujitokeza ambapo watu waliokuwa wamepanga kufanya shughuli mbalimbali wamezifuta. Mama mmoja, Mwajuma Juma aishie eneo la Majevu jirani na hospitali ya wilaya alishindwa kufanya Maulidi yake baada ya kukosa shilingi 5000 za kulipa ofisi ya Bakwata. Mama huyo alikuwa amenuia kusoma Maulidi kumshukuru Mungu baada ya mtoto wake aliyekuwa amepata ajali kupona. Kushindwa kupata elfu tano hizo, mama huyo alifanya tafrija ndogo ya chai kwa majirani na ndugu zake. Hata hivyo kwa kukosekana Maulidi vijana hawakuona mantiki ya tafrija hiyo kufanywa kimya kimya, kwahiyo wakaiteka nyara na kupiga disko. Baadhi ya majirani Waislamu nao hawakuridhika na hali hiyo ya kuigeuza hafla ya kumshukuru Mungu kuwa ya disko, walimuomba mama muhusika disko lisimamishwe wasome dua, ambapo walisoma. Uchunguzi zaidi umebaini kwamba Waislamu mjini Same wanaandaa utaratibu wao wa kuendesha shughuli zao za Khitma, Dua, Maulidi na ndoa kupitia taasisi nyingine za Kiislamu ambazo haziwatozi mapato. Kwa ujinga baadhi ya waumini wamekuwa na fikra potofu kwamba ibada zao na mambo kama mazishi, kuozesha, dua, maulidi n.k. hayawezi kuswihi mpaka yafanywe na Sheikh maalum au chombo maalumu cha kidini. Hali hiyo imewapelekea wanaokabidhiwa jukumu la kuzifanya shughuli hizo kuweka viwango vya malipo ambavyo vinajenga hisia za kujali chumo zaidi kuliko huduma. Malalamiko ya Waislamu yatokanayo na hali hii yataondoka tu pale Waislamu
watakapo elimika wajue kwamba wanaweza kumwombea dua maiti wao bila ya
kumsubiri Sheikh maalum na kwamba Walii anayeozesha binti ni baba mzazi
(au kaka, babu nk) na wala sio Sheikh wa taasisi fulani.
|
YALIYOMO
TAHARIRI Majeshi ya nje kupelekwa Lesotho: Je, ni sera za Nguvumali? Nyumba ya Wakfu yageuzwa Baa
Dar
‘VAT’ yaingia Bakwata Same
Mchungaji asema hakuna mihadhara ya
kashfa
Maoni yetu: Masheikh tupeni Fatwa Safari yangu Ufini
Unyanyasaji wa kidini mashuleni, vyuoni
ukomeshwe
Wanaume toeni haki za wanawake
MAONI: Yesu ni yule yule Isa
Hatuna uwezo wa kuwapinga manabii
Ukoloni mwingine unaingizwa
nchini?
Khatamy ni ‘Gorbacheiv’ mwingine?
Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo
kwa maneno
AN-NUUR lina chuki na
Wakristo
Msiiparamie ovyo Biblia
Yaliyosemwa na viongozi wa dini juu
ya idadi ya watu 1989
Uislamu ulivyoingia Zanzibar -2 Waislamu Moro watakiwa kutoyumba
Wanawake Masasi wawataka Masheikh
kutangaza sheria za Allah
Ugaidi na Uislamu siyo kitu
kimoja – Sheikh Jongo
Sheikh Abbas awataka wananchi
Dodoma waepuke upuuzi
Vijana watakiwa kujiepusha
na ‘vijiwe’
Mafundisho ya Quran
Chakula na Lishe
|