|
|
|
Na Mwandishi Wetu NYUMBA iliyokuwa imewekwa Wakfu na marehemu Hajat Aziza Omar inadaiwa kuchukuliwa na Bw. Daniel Zakaria ambaye naye amemuuzia Bw. Pius Kipengele. Nyumba hiyo No. 58 iliyopo Mtaa wa Somali sasa imewekwa baa. Nyumba nyingine No. 59 iliyopo Mtaa wa Mchikichi nayo inadaiwa kuchukuliwa na huyo huyo Bw. Daniel na kisha kumuuzia Bw. Steven Mwamkoa. Kwa mujibu wa maelezo ya wadhamini wa Masjid Mwinyi, nyumba hizo mbili zilikuwa za Hajat Aziza Omar na alizitoa Wakfu kwa Msikiti kwa hati ya kiapo MCA 284 2/84 ya Oktoba 11, 1990 katika mahakama ya Mwanzo Kariakoo. Katika hati hiyo ya kiapo Hajat Aziza Omar wakati huo akiishi katika nyumba No. 58 Mtaa wa Somali aliithibitishia mahakama kwamba hana udugu wa damu wa kumrithi na hivyo akasema: "Natoa wosia kwamba nikifa nyumba hizo ziwe Wakfu kwa ajili ya Masjid Mwinyi uliopo Na. 66 Moshi St. Ilala Dar es Salaam". Msikiti huo Masjid Mwinyi aliujenga yeye Hajat Aziza kwa kuvunja nyumba yake iliyokuwa Ilala ili kiwanja hicho ujengwe Msikiti. Aidha, fedha zilizojengea Msikiti huo alizitoa yeye baada ya kuuza nyumba yake nyingine iliyokuwa Mtaa wa Agrey. Hajat Aziza bint Omar alifariki Mei 5, 1991 ambapo wasimamizi wa Wosia wake walikwenda mahakamani kutoa tangazo la Usimamizi wa Mirathi, tangazo hili lilitoka katika gazeti la UHURU la Ijumaa Septemba 13, 1991, likieleza kwamba Shauri litasikilizwa Desemba 10, 1991 na kwamba Wosia wa marehemu upo mahakamani, hivyo waweza kukaguliwa na yeyote. Baada ya kutokutokea yeyote kupinga Wosia huo, Januari 23, 1992 Mahakama ya Mwanzo Kariakoo ilitoa haki ya kusimamia mirathi hiyo kwa waombaji. Hata hivyo katika rejea ya shauri la madai No. 3 la 1993 Hakimu Natalia Kimaro alitoa haki ya kusimamia nyumba hizo kwa Bw. Daniel Zakaria. Hoja iliyozingatiwa na mahakama hiyo ni kwamba Bw. Daniel aliomba usimamizi wa Mirathi ya Hajat mahakama ya Kisutu Septemba 6, 1991. Kwamba tangazo la Mirathi hiyo lilitolewa katika gazeti la Serikali (Government Gazette) No. 469 la Septemba 20, 1991 na Bw. Daniel kupewa kibali Desemba 22, 1991 na mahakama ya Kisutu. Toka hukumu hiyo itolewe Waislamu wa Masjid Mwinyi wamekuwa wakikata rufaa mahakamani, lakini mpaka hukumu ya mwisho ilipotolewa na Jaji J.M. Mackanja Mei 12, 1998 bado mahakama inamtambua Bw. Daniel kama msimamizi wa nyumba hizo. Hukumu hiyo ya Mei 12, mwaka huu ilitolewa bila ya mawakili wa pande zote mbili kuwepo mahakamani. Kwa mujibu wa vielelezo ambavyo AN-NUUR inavyo, hakuna mahali ambapo uhalali wa kiapo cha Wakfu umehojiwa. Aidha, Masjid Mwinyi bado wanalipia kodi ya majengo kwa nyumba hizo. Mei 1, 1996 Halmashauri ya Jiji iliwaandikia Masjid Mwinyi kutaka walipe kodi ya nyumba No. 59 ambayo ilikuwa shilingi 5700, kodi hiyo ililipwa Julai 30, 1996 na wakapewa stakabadhi Na. 0570256. Aidha, Aprili 29, 1997 Tume ya Jiji iliwaandikia Masjid Mwinyi walipe kodi ya shilingi 10,000 ya nyumba hiyo ambapo walilipa Juni 23, 1997 na kupewa stakabadhi Na. A00117860. Wadhamini wa Masjid Mwinyi waliwahi kulalamika serikalini (ofisi ya Rais) wakionyesha jinsi wasivyoridhika na mwenendo wa shauri hili katika mahakama. Katika malalamiko yao ya maandishi kwa Rais, walidai kwamba Bw. Daniel alifanya hadaa. Badala ya kupinga Mirathi waliyofungua mahakama ya Kariakoo yeye alifungua nyingine katika mahakama ya Kisutu. Lakini zaidi ya hivyo, akaitangaza mirathi hiyo katika gazeti la Serikali ambalo hakuna mwananchi wa kawaida anayelisoma. Aidha, wamelalamika kwamba ni vipi Bw. Zakaria anapewa haki ya kurithi nyumba za Wakfu wa Muislamu wakati sheria ya Mirathi ipo wazi kwamba Muislamu kwa namna yoyote hawezi kurithiwa na Mkristo. Na zaidi hawana udugu kabisa, si wa damu wala wa kuoleana. Aidha, wamelalamika kwamba baada ya hukumu ya Hakimu Natalia Kimaro walikata rufaa Mahakama Kuu chini ya Jaji Mapigano na ikashauriwa shauri lirudishwe mahakama ya Kisutu ili Hakimu aliyeamua shauri hilo bila kusikiliza upande wa pili apate nafasi ya kuwasikiliza Waislamu. Hata hivyo wamedai kwamba mahakama hiyo haikuisikiliza kesi hiyo na
wakashangaa kuletewa hukumu kutoka Mahakama Kuu kwa Jaji huyo huyo D.P.
Mapigano (Februari 25, 1994) ikitupilia mbali ombi lao la rufaa kinyume
na agizo la awali kwamba isikilizwe.Kutokana na hukumu hiyo, Bw. Daniel
Zakaria ashaivunja nyumba ya Mchikichi sasa ni kiwanja kinasubiri kujengw
Juhudi za gazeti hili kumpata Bw. Daniel kuzungumzia suala hili hadi tunakwenda
mitamboni hazikuweza kufanikiwa.
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Nyumba ya Wakfu yageuzwa Baa
Dar
‘VAT’ yaingia Bakwata Same
Mchungaji asema hakuna mihadhara ya
kashfa
Maoni yetu: Masheikh tupeni Fatwa Safari yangu Ufini
Unyanyasaji wa kidini mashuleni, vyuoni
ukomeshwe
Wanaume toeni haki za wanawake
MAONI: Yesu ni yule yule Isa
Hatuna uwezo wa kuwapinga manabii
Ukoloni mwingine unaingizwa
nchini?
Khatamy ni ‘Gorbacheiv’ mwingine?
Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo
kwa maneno
AN-NUUR lina chuki na
Wakristo
Msiiparamie ovyo Biblia
Yaliyosemwa na viongozi wa dini juu
ya idadi ya watu 1989
Uislamu ulivyoingia Zanzibar -2 Waislamu Moro watakiwa kutoyumba
Wanawake Masasi wawataka Masheikh
kutangaza sheria za Allah
Ugaidi na Uislamu siyo kitu
kimoja – Sheikh Jongo
Sheikh Abbas awataka wananchi
Dodoma waepuke upuuzi
Vijana watakiwa kujiepusha
na ‘vijiwe’
Mafundisho ya Quran
Chakula na Lishe
|