|
|
Majeshi ya nje kupelekwa Lesotho: HIVI karibuni majeshi ya Afrika Kusini na ya Zimbabwe yaliivamia nchi ya Lesotho ambayo kijiografia imezungukwa na Afrika ya Kusini kwa madai kuwa majeshi hayo yamepelekwa huko kwa kuombwa na nchi za SADCC ili yakamalize mgogoro wa kisiasa uliosababishwa na vyama vya upinzani kutotambua matokeo ya uchaguzi uliofanyika huko mwaka huu. Kwa maoni yetu tunadhani uamuzi huu wa nchi za SADCC unasikitisha na unastahiki kukemewa kwa sababu unaimarisha mtazamo potofu kuwa "mwenye nguvu ndiye mwenye haki na mnyonge hana haki yoyote". Tunafahamu kuwa hali halisi ya siasa za dunia yetu hivi leo, kama ambavyo imekuwa katika vipindi virefu vya historia ya binadamu, inatawaliwa na kanuni ya "Nguvumali" yaani fikra kuwa anachosema, anachotenda au kuamrisha mtu au taifa lenye mabavu ndicho cha kweli na cha sawa! Dhulma kwa binadamu na ufisadi katika ardhi vinakuwa ndio haki za binadamu ikiwa mbabe atasema ufisadi huo ni haki, na watu wote watatakiwa wakiri na kutekeleza amri na matamshi ya mbabe hata kama ni yenye kuangamiza. Mifano ipo mingi. Hivi leo watu wa dunia nzima wanashinikizwa wakubali kuwa liwati, ushoga, kutoa mimba, kuwafundisha watoto wadogo ngono na kuwapa kondomu, na kumwacha mtoto afanye apendacho bila kumrudi ndio haki za binadamu!. Hivi leo nchi zenye nguvu kubwa kijeshi zinazisakama nchi changa zinazotaka kumiliki silaha za nyuklia, ilhali wao wenyewe wanazo! Nchi zenye nguvu kubwa kiuchumi zinatulazimisha kuwa raia wetu hata wakiwa mafakiri vipi serikali isiwape matibabu hata kama wanaumwa vipi, na wafe tu, ilhali wao katika nchi zao raia wote wana haki ya kutibiwa na hata kupewa posho ya kuwakimu! Hayo yote tunayajua, lakini tunaendelea kuamini kuwa ukweli na haki havitegemei ubabe wa mtu au taifa. Ukiizingatia migogoro ya kisiasa iliyomo katika nchi wanachama wa SADCC na namna nchi hizo zinavyoishughulikia migogoro hiyo utaona dhahiri kuwa Lesotho imeingiliwa kijeshi kwa sababu tu ni nchi nyonge kijeshi na kiuchumi. Angalau Lesotho kuna vyama vya siasa vya upinzani jambo ambalo haliruhusiwi huko Uganda, lakini Uganda hiyo hiyo imeshiriki katika maamuzi ya kupelekwa majeshi Lesotho! Uganda sio tu imejiingiza kijeshi katika nchi ya Kongo, lakini ni katika nchi wanachama wa SADCC zinazomtaka Rais wa Kongo afanye mazungumzo na waasi, ilhali yeye mwenyewe anayo makundi matatu yanayompinga kijeshi na hayupo tayari kufanya nao mazungumzo! Utata huo upo katika nchi nyingine ikiwemo nchi yetu ambayo mpaka hivi bado haijaweza kuutatua mgogoro wa uchaguzi wa 1995 kwa upande wa Zanzibar. Huko nyuma Tanzania ilikuwa ni miongoni mwa nchi zilizoishutumu sana Marekani kwa kujiteua yenyewe kuwa ndio polisi wa dunia. Lakini katika ubabe ulioonyeshwa na Marekani hivi majuzi Tanzania haikuipongeza Marekani kwa kuzishambulia kijeshi Sudan na Afghanistan, lakini pia haikuthubutu hata kuilaumu japo kwa mbali! Kama SADCC ndiyo iliyoishauri Lesotho ivamiwe kijeshi maana yake nchi yetu pia imeshiriki katika maamuzi ya kuziomba Afrika Kusini na Zimbabwe ziingilie kijeshi Lesotho. Kama raia wa nchi hii ya Tanzania tunaishauri nchi yetu itafakari vizuri siasa zake za nje. Na hilo litawezekana tu kwa kuwa na mwelekeo unaoeleweka katika siasa zetu za ndani. Tunaamini kuwa ni makosa makubwa kudhani kuwa mataifa dhaifu kijeshi au kiuchumi hayastahili kutendewa haki kama ambavyo ni makosa kuwanyima haki raia ambao ni wanyonge katika nchi. |
YALIYOMO
TAHARIRI Majeshi ya nje kupelekwa Lesotho: Je, ni sera za Nguvumali? Nyumba ya Wakfu yageuzwa Baa
Dar
‘VAT’ yaingia Bakwata Same
Mchungaji asema hakuna mihadhara ya
kashfa
Maoni yetu: Masheikh tupeni Fatwa Safari yangu Ufini
Unyanyasaji wa kidini mashuleni, vyuoni
ukomeshwe
Wanaume toeni haki za wanawake
MAONI: Yesu ni yule yule Isa
Hatuna uwezo wa kuwapinga manabii
Ukoloni mwingine unaingizwa
nchini?
Khatamy ni ‘Gorbacheiv’ mwingine?
Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo
kwa maneno
AN-NUUR lina chuki na
Wakristo
Msiiparamie ovyo Biblia
Yaliyosemwa na viongozi wa dini juu
ya idadi ya watu 1989
Uislamu ulivyoingia Zanzibar -2 Waislamu Moro watakiwa kutoyumba
Wanawake Masasi wawataka Masheikh
kutangaza sheria za Allah
Ugaidi na Uislamu siyo kitu
kimoja – Sheikh Jongo
Sheikh Abbas awataka wananchi
Dodoma waepuke upuuzi
Vijana watakiwa kujiepusha
na ‘vijiwe’
Mafundisho ya Quran
Chakula na Lishe
|