| AN-NUUR
lina chuki na Wakristo
Na Charles
Kamuhabwa, DSA Mtwara
MIMI ni msomaji mzuri wa gazeti la AN-NUUR, jambo nililogundua katika
siku zote hizi za kulisoma gazeti hili ni kuwa Mhariri wa gazeti hili pamoja
na wachangiaji wengi wa makala mbalimbali katika gazeti hili wana chuki
zisizo za msingi na Ukristo pamoja na Wakristo wenyewe kwa ujumla.
Sioni ni kwa sababu gani gazeti hili kuchukua nafasi kubwa na muda mwingi
kuukosoa, kuulaumu, kulaani na hata kuukashifu Ukristo. Kinyume kabisa
na mafundisho ya Qur’an inayosema katika moja ya aya zake kwamba "Hakuna
watu walio karibu yenu zaidi ila ni wale wasemao sisi ni watu wa Kitabu".
Badala yake gazeti la AN-NUUR kwa sababu mnazozijua wenyewe mmekuwa
mnauandama Ukristo na Wakristo kama vile Qur’an imewaambia "hakuna watu
walio adui zetu ila ni wale waliosema sisi ni watu wa kitabu".
Kila kitu kinachohusiana na Ukristo iwe ni utawala au mtawala, taasisi,
elimu na hata kitabu chetu kitakatifu Biblia hupigwa vita na kutuliwa kila
aina ya lawama.
Kwa mfano, pamoja na huduma nzuri za hospitali zitolewazo na taasisi
nyingi za Kikristo katika mikoa ya Kusini (Lindi na Mtwara) kuna wakati
mchangiaji mmoja wa makala zako alipoitaka serikali kuwatoza kodi Wamisionari
wanaoagiza dawa kwa ajili ya hospitali za Ndanda, Nyangao na nyinginezo
nyingi.
Hivi mtu huyo anafahamu kuwa hospitali hizi ndio tegemeo kubwa la wananchi
wa sehemu hizi? Ambao karibu 80% ni Waislamu? Je, ni taasisi gani ya Kiislamu
ambayo imechukua angalau hatua ya kuwajengea hata ki-dispensary watu hawa
au chuki tu dhidi ya Ukristo inaweza kumpasua mama mjamzito anayehitaji
huduma hii? Au angalau kumpasua mzee mshipa?
Mfano mwingine ni utawala wa kikoloni (Wajerumani na Waingereza) hulaumiwa
kuwa kwa kuwa walikuwa Wakristo ndio chanzo cha Waislamu wa nchi hii kuwa
nyuma kimaendeleo katika nyanja za elimu, uchumi na afya, lakini cha ajabu
gazeti hili halijawahi kutuambia kuwa Waarabu (Waislamu) ambao ndio wa
kwanza kufika na kutawala mwambao huu wa Pwani ya Afrika Mashariki kabla
ya hao Wajerumani na Waingereza wameacha wamewafanyia nini Waislamu wa
sehemu hizi katika nyanja zilizotangulia hapo juu yaani elimu, uchumi na
afya?
Mbali ya kuwapeleka mamilioni utumwani ambao hadi hivi leo hatujui vizazi
vyao vimepotelea wapi.
Pili, si siri kuwa ni Waarabu hao hao ambao waliwazuia wananchi wa maeneo
haya (Waislamu) kupeleka watoto wao shule kwa visingizio vya "watakula
nyama za nguruwe" au kufundishwa Injili.
Matokeo yake Waislamu wengi wa maeneo ya Mwambao wa Afrika Mashariki
hawakuwapeleka watoto wao shule hata kama shule zenyewe zilikuwa za serikali.
Wengine walifikia hata hatua ya kufikishwa mahakamani na wakoloni hao hao.
Sasa wa kulaumiwa hapo kuwa alirudisha nyuma maendeleo kielimu ya watoto
hao ni nani, Waingereza na Wajerumani au Waarabu? Matunda ya hatua hiyo
ndio huko kubaki nyuma kielimu kwa watu wa sehemu hizi.
Sasa basi nakuomba Mhariri wa AN-NUUR na watu wengine wanaokuunga
mkoni mnieleze kupitia gazeti hili maendeleo yoyote ambayo watu wa Afrika
Mashariki tunaweza kujivunia kuwa tumepata kutoka kwa utawala wa miaka
mingi wa Waarabu katika Pwani ya sehemu hii (tangu enzi za Seyyid Said)
mbali ya magofu ya masoko ya watumwa na kuandika kombe (mijarabati).
Hatuoni angalau hata Msikiti ambao mtu anaweza kusema ulijengwa na Waarabu,
achilia mbali shule, daraja au barabara. Pili Waislamu wenzenu wa Zanzibar
ambao wao ndio waliotawaliwa zaidi na Waarabu na hawakuonja utawala wa
Wajerumani na hata huo wa Waingereza ulikuwa kupitia kwa Sultani wa Kiarabu
wana maendeleo gani kielimu, afya na uchumi zaidi yenu nyinyi mliotawaliwa
na wakoloni hao (Wajerumani na Waingereza)?
Kuhusu madai kuwa Waislamu wa Tanzania wana haki ya kulipwa fidia na
Wajerumani na Waingereza vipi kuhusu Waarabu mimi nadhani wao ndio wanaopaswa
kulipa fidia kubwa zaidi. Thamani ya mwanadamu ni shilingi ngapi? Ndugu
zetu waliobebwa na kupelekwa utumwani wakapotelea huko watalipwa na nini?
Kama tendo la kukusanya kodi, mazao na maliasili yetu kulikofanywa na
Wajerumani na Waingereza kunatakiwa kufidiwa vipi maisha ya mababu na bibi
zetu? Vipi pembe za ndovu? Na utajiri mwingine walio ubeba Waarabu? Nadhani
AN-NUUR mtanipa jibu zuri kuhusu maswali haya.
Nchi nyingi za Ulaya hasa zile za Nordic hivi sasa zinaongoza katika
kutoa misaada bila ubaguzi wa kidini kwa nchi yetu lakini sikia msaada
ukitoka Uarabuni unakuwa na vikwazo lazima upelekwe kwa Waislamu au taasisi
ya Kiislamu. Je, hizi nchi za Nordic (Wakristo) nao walituchukulia nini?
Au wamewahi kuitawala nchi hii?
Waislamu wengi wanaochangia makala katika gazeti la AN-NUUR hupenda
kuwasadikisha Waislamu pamoja na wasomaji wote kuwa Biblia si kitabu cha
Mwenyezi Mungu, imebadilishwa badilishwa, imepunguzwa na kuongezwa mambo
mengi ambayo wala hawatoi ushahidi kuwa mambo hayo ni yepi.
Lakini hawasemi lolote kuhusu hadithi za Kiislamu zilizotolewa na kuandikwa
na Waislamu wenyewe (sio Wakristo) kwamba hata Qur’an yenyewe imepunguzwa
punguzwa. (Tazama sahihi Bukhari mlango wa Ash-Shahada Takunu Indal Hakim
Fii Wilayatihi Qaadhaa katika Al-Alkaani) utaona hadithi isemayo kwamba
Umar bin Khatab (Khalifa) amesema: "Lau kama si kuogopa watu kusema Umar
amezidisha (kitu) katika kitabu cha Mwenyezi Mungu ningeliandika aya ya
Rajm kwa mikono yangu mwenyewe". Je, hii si kuonyesha kuwa Qur’an pia imepunguzwa
baadhi ya aya zake maana aya hiyo ya Rajm hivi sasa haimo kwenye Qur’an
tuliyo nayo.
Soma pia sahihi Bukhari mlango Wamaa Khalkadh Wal Unthaa katika Kitabut
Tafsir utaona kuwa hapo mwanzoni Qur’an sura 92:3 ikisomwa tofauti na leo.
Aya Alqama anasema walikuwa wakiisoma hivi "Wadh Dhakari Wal Unthaa" anaendelea
kusema, "ninashuhudia kwamba nimesikia Mtume (saw) akisoma hivi: "Ila hawa
(baadhi ya masahaba) wanataka nisome: "Wamaa Khalaqadh dhakara wal unthaa".
Naapa kwa jina la Mwenyezi Mungu sitawafuata".
Pia kuna hadithi nyinginezo nyingi zisemazo kuwa Qur’an tuliyo nayo
hivi sasa ni hadithi tu (1/3) ya ile ya asili Hii inaonyesha kuwa masahaba
wa Mtume Muhammad (saw) (hasa makhalifa) waliondoa au kuongeza waliyoyataka
katika Qur’an maana Qur’an hapo mwanzo hakuandikwa (enzi za Mtume) ilikuwa
ikihifadhiwa moyoni sasa kumbukumbu za binadamu kama tunavyozijua mwambie
leo "pi" leo kesho atasema "pa".
Ushahidi mwingine ni kutoka kwa Ibn Umar mwenyewe angalia Al Itqan (juzuu
ya pili Uk. 32) utaona imeandikwa kuwa imepokewa kwa Nafi kwamba Ibn Umar
amesema "Huenda mmoja wenu akasema kwamba ameichukua Qur’an yote (ukweli
ni kwamba ) Qur’an nyingi imetoweka lakini aseme nimeichukua sehemu iliyodhihiri
(niliyoipata)".
Sasa mheshimiwa Mhariri wa AN-NUUR hayo mbona huwa hamtuambii au Waislamu
wote wanayajua kuna baadhi ya Waislamu hapa Mtwara hata hao Makhalifa wenyewe
hawawajui ila Paulo. Oh wanamjua sana mpaka historia yake.
Kuna mambo mengi yanayofanywa na Waislamu wengi siku hizi lakini hayakuwepo
enzi za Mtume (saw) wala hayamo kwenye Qur’an kama Maulidi ya Uzawa wa
Mtume, Kudhikiri, kuswali Taraweih jamaa na mengine mengi yameanzishwa
au kubuniwa na masahab haswa (makhalifa).
Hayo AN-NUUR hamyasemi wala hamyaelezei ingawaje mara kwa mara yanaleta
migongano miongoni mwa Waislamu wa madhehebu mbalimbali.
Siwezi kuitetea Biblia kuwa imepunguzwa au kuongezwa ongezwa lakini
na jua moja tu ndio kitabu sahihi kuliko vyote duniani. Hata Waislamu mna
haki ya kuiona hivyo Qur’an yenu sasa hizi kelele zote za "Biblia imepunguzwa"
za nini? Maana kinachotakiwa ni kufuata amri za Mwenyezi Mungu na mapenzi
yake.
Sasa basi ni vyema AN-NUUR na wote wanaoona kuwa Uislamu ndio bora kuliko
dini nyingine zote ndio ufuatao sheria za Mungu, Kitabu chenu hakikubadilishwa
na Nabii wenu ndiye Mkuu kuliko wote mtujulishe ni nini kilichopelekea
Waislamu kuuana wenyewe kwa wenyewe mara tu baada ya kifo cha Mtume? Ni
kwanini Mzee wa miaka zaidi ya 80 Seyyid Uthman (Khalifa) aliuawa kikatili
Msikitini akiwa kwenye sala? (Taz. Maisha ya Seyyid Uthman).
Uislamu ni nini? Maana ubora wa dini huonekana kwenye waumini wa dini
yenyewe. Sasa mbona hatuoni tofauti katika maisha ya Waislamu na watu wengine
wasio Waislamu kama Wakristo (ambao dini yao si bora kama yenu). Sasa huo
Uislamu upo hapa duniani au mbinguni? Kama vile Wakristo kuua Waislamu
walevi, wazinzi, wadhulumaji, wafitini, waongo na zaidi ya yote washirikina
wakubwa.
Ukitaka kuroga timu ya mpira ishinde nenda kwa Sheikh akusomee kitabu,
ukitaka kumtia mtu uwendawazimu nenda kwa mwalimu wa Kiislamu (akuandikie
kombe), ukitaka hata kuua nenda kwa mtaalamu wa Kiislamu akuandikie au
amsomee huyo mbaya wako Albadiri.
Tazama sehemu zote zenye wakazi wengi ni Waislamu sehemu za Pwani, Bagamoyo,
Tanga, Zanzibar, Mtwara (mikindani) na Mombasa mtajie mtu miji hiyo halafu
muulize sifa yake kubwa nini. Miji hiyo kama sio ushirikina. Sasa ubora
wa Qur’an na Uislamu wake dhidi ya diin nyinginezo uko wapi?
Badala ya kuuandama Ukristo na habari za Mwana wa Mungu, kula nguruwe,
kusali na viatu, bassi kwanza warekebisheni hao wenzenu niliowataja hapo
juu.
AN-NUUR, wahadhir wa Kiislamu wote na mtu mwingine yeyote yule ajue
aya hii: "Watendao maovu wote, wawe ni Waislamu, Wakristo na wengineo wote
sehemu yao ni jehanamu ya moto".
Bwana Yesu anasema "Si wote wasemao Bwana Bwana wataingia ufalme wa
Mungu. Wale watendao maovu nitawakataa na kusema siwajui nyinyi mtokako
nendeni zenu motoni".
Na Mtume Muhammad (saw) anasema "kundi la sahaba wangu litanijia siku
ya kiama lakini watafukuzwa kwenye hodhi; hapo nitasema Ewe Mola wangu
(hao) ni sahaba wangu. Naye atasema hajui walizua nini baada yako. Wao
walirejea nyuma kwa visigino vyao". Hadithi nyingine inasema ingawa Mtume
(saw) aliwatambua kwa alama za swala kwenye vipaji vya nyuso zao, lakini
anaongezea kuwa "Basi sikuwaona yoyote miongoni mwao aliyesalimika isipokuwa
(wachache) mfano wa ngamia wasio na mchunga."
Sasa ndugu yangu hapa Bwana Yesu na Muhammad (saw) wanatuonyesha kuwa
siku hiyo si dini yako wala Nabii wako watakaokuokoa na moto kama ulikuwa
mtenda maovu. Ila kila mtu atatoa habari zake mwenyewe! Kama Mtume hataweza
hata kuwatetea sahahaba zake je wewe mwenzangu? Si hivyo tu Mtume Muhammad
(saw) kasema kumwambia mwanawe (Fatma) kwamba atende mema. Yeye hana msaada
wowote kwake mbele ya Mungu.
Tunaishika Biblia yetu ishikeni Qur’an yenu tukutane mbele ya Kiti cha
Hukumu!
Msiiparamie
ovyo Biblia
Na Sheikh
Bernard P. Nyangasa
NIMEKUWA nikisoma makala mbalimbali za kidini (Ukristo) katika magazeti
mbalimbali zikijaribu kuthibitisha au kukanusha madai mbalimbali. Nimegundua
kuwa waandishi wengi hawana elimu ya theologia hasa masomo ya Bible
Knowledge na Church History. Waandishi hawa wanaandika vitu
visivyo na kichwa wala miguu. Wanaandika kile wanachosikia Makanisani na
kwenye mikutano ya dini bila kujua kuwa wanachosikia hakimo katika vitabu
vitakatifu wala vitabu vya theologia.
Vitu vingine hata havihitaji elimu kuvigundua kuwa ni upuuzi. Maneno
kama "Isa sio Yesu" ni upuuzi! Nikimwambia mtu huyo kuwa Yesu sio Yehoshua
atakubali? Kwani Yehoshua (maana yake Bwana aokoa) ndio jina asili la Yesu
la Kiebrania alilotumia.
Hapa nitatoa mfano mmoja tu wa Bwana Eliya Batendi. Nimechagua barua
yake: "Ujumbe kwa waandishi" (AN-NUUR No. 164) kwa kuwa ina ‘wimbo
wa taifa’ ambao unaimbwa katika Makanisa yote duniani na unaaminika ndio
‘wimbo sahihi wa taifa’.
Bwana Batendi anasema: " watu hawa hawawezi kunukuu Isaya 9:6 Tumepewa
mtoto mwanamume (Yesu) ataitwa Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu".
Kwanza naomba ili tuendelee na kipengele hiki, tujifanye hatujasoma
Topic ya nyakati (tense) katika somo la sarufi (Grammer.) Kwani
tukijifnya tumesoma somo hilo tutakwamia hapa hapa.
Tuangalie watalaamu wa Biblia (Wanatheologia) wanasemaje "9:1. Inaonekana
kuwa ni utangulizi wa uaguzi ulio katika aya zifuatazo. Uaguzi ulitabiriwa
wakati Wagalatiya walipohamishwa na Tiglath – Pileseri wa tatu Mfalme wa
Ashura mwaka 732 K.K. Uaguzi huo unatangaza "siku ya Bwana" (AMO 5:18).
Siku ya Bwana itawakomboa waliohamishwa na kuwaletea ufalme wa amani atakaoshika
mtoto wa ukoo wa kifalme. Mtoto huyo haikosi ni Immanuel anayetajwa katika
7:14. Kufika kwa Kristo Galilaya watatimiza uaguzi huo (Mt. 4:13016) "
Tazama Biblia Takatifu Tabora Uk. 658. Hapo tunaelekezwa kuwa Isaya 9:1-7
inahusiana na Isaya 7:14 isemayo "Kwa hiyo BWANA mwenyewe atawapa ishara.
Tazama bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume naye atamwita jina
lake Immanueli".
Hapa ‘wimbo wa taifa’ tunaousikia kila siku ni kuwa Immanuel ni Yesu
na bikira ni mama Maria. Sasa tuzame ndani sana katika vyuo vya theologia
ili kujua kweli huo ni ‘wimbo sahihi wa taifa?’
Hapa nanukuu kitabu kimojawapo ambacho ni mwongozo kwa walimu wa theologia
(Teacher’s guides to religions education series) uliokubaliwa na Wanatheologia
wote (Agreed Sylabases).
Kitabu hiki kinaitwa "The Rise the Prophets" Senior lessons – Volume
Six cha Norman J. Bull, M.A – Champlain and lecturer in Divinity Saint
Luke’s College. Mfululizo wa miongozo hii imetayarishwa na The Religious
Education Press Ltd.
Wallington Survey (1961) katika ukurasa wa 156 kikizungumzia "Imanuel"
kinasema "(b) Immanu-el. It was Isaiah’s Unwavering Conviction that Yahweh
was with His people – Immanu-el (God with us) – If they would but put their
whole trust in Him. The Prophet offered a sign of this to the weak and
wavering Ahaz (see above). A ‘Young woman’ – not ‘ a virgin’ – was with
child, and would bear a son to be called Immanu-el. Before he was old enough
to know good from evil, Israel and Syria will have been destroyed. This
‘sign’ is given in a concrete historical situation (7:14, 8:8,10 cf. Rom
8.31); it is not visionary future possibility. The ‘young woman’ may well
have been Isaiah’s own wife (ef. 8:3) or even the wife Ahaz. From the point
of view of Isaiah, there is no Prophecy here of a virgin birth".
Hicho ndicho wanachofundishwa Makadinali, Maaskofu, Mapadre n.k. kuwa
huyo mwanamke hakuwa bikira (not a virgin) na tayari alikuwa na mtoto (was
with child) na wala sio Maria bali mke wa Nabii Isaya au mfalme Ahazi.
Na wanasisitiziwa kuwa hakuna utabiri wa uzazi wa mwanamke bikira hapo
" there is no Prophecy here of a virgin birth".
Hii ingawa inashangaza sana, lakini ndio ukweli wenyewe. Kwani neno
asili la Kiebrania lililotumika hapo ni "Almah" yaani mwanamke bikira au
mwanamke aliyeolewa karibuni hata kama alikuwa mjane mwenye watoto sita.
Hivyo kwa kuzingatia na mapokeo mengine ya Kiebrania na Kiaramu (hayamo
katika Biblia) tafsiri sahihi hapo ni hiyo ya pili, ingawa ‘wimbo wa taifa’
ni tafsiri ya kwanza. Sasa tuondoke huko kwenye vyuo vya watu tunamrudia
Bwana Batendi.
Bwana Batendi anasema: "Wakati Yesu anaagiza lianzishwe Kanisa Mathayo
16:18 alikuwa na maana waswali humo Waislamu? Inaonekana huyu Bwana (pamoja
na wengine) anadhani Kanisa alilozungumzia Yesu ni jengo.
Tuwaachie wataalamu wetu watusaidie. "16:18 Neno Kanisa lilivyoeleweka
katika nchi za Mashariki ni mkutano. Katika Agano la Kale mara nyingi Kanisa
ni jumuiya ya wateule, hasa taifa takatifu jangwani (Mdo. 7:38) Yesu atumia
neno hili Kanisa katika maana ya jumuiya ya Kimasiya atakayofanya nayo
Agano Jipya kwa kumwaga damu yake (26:28, Efe. 5:25).
Pengine Kanisa kadiri ya Yesu ni kama Ufalme wa Mbinguni (9:19, 4:17).
Ni jumuiya ya "Nyakati za Mwisho" itakayoanza hapa duniani ikiendeshwa
na Katiba na Mkuu wake (Mdo. 5:11)" Tazama Biblia Takatifu Tabora Uk. 894.
Bwana Batendi anaendelea kusema: "Wakati Yesu anawatuma wanafunzi wake
waende duniani kote, wawafanye watu kuwa wanafunzi wa Yesu, wawabatize
kwa jina la Baba la Mwana na Roho Mtakatifu (Mathayo 28:19) alikuwa na
maana Waislamu wabatizwe? Huyu Bwana kama ilivyo kwa Wakristo wengine (wasio
wanatheologia) anadhani "ubatizo" ni kumwagiwa maji kichwani au kutoswa
majini. Maana ya ubatizo ni hii ifuatayo:
"6:4 Watu wa zamani hubatizwa kwa kutoswa majini, na maana ya neno la
ubatizo kwa Wayunani ni kutosa majini ubatizo kadiri ya Biblia una habari
zaidi ya huko kufa na kufufuka katika Kristo pengine una maana ya kumtakasa
mtu (Efe. 5:26, Ebr. 10:22).
Pengine ni kuzaliwa kupya (Yn 3:5, Tit 3:5), pengine ni kuangazwa kupya
(Ebr 6:4, 10:32), kadiri ya 1 Pet. 3:21 Safina ya Nuhu ni mfano wa ubatizo".Biblia
Takatifu Tabora Uk. 1032.
Wanatheologia wanatufahamisha zaidi kuwa hata Wapagani nao walikuwa
wanabatiza. "3:6 Ibada ya kutosa mwili ni mfano wa utakaso au wa kujitengeneza
upya. Ibada kama hiyo ilijulikana na kutendeka katika dini za kale za Kipagani
na dini ya Kiyahudi pia (kama ubatizo wa waongofu. Mdo. 2:10, Waesseni)"
BTT Uk. 879 Yesu mwenyewe japo alishabatizwa (Mt. 3:16) bado alikabiliwa
na "ubatizo" mwingine aliouhofia sana. "Nimekuja kutupa moto duniani, na
ukiwa umekwisha washwa, ni nini nitakalo zaidi? Lakini nina ubatizo unipasao
kubatizwa, nami nina dhiki kama nini hata utimizwe (Luka 12:49 – 50).
Bwana Batendi na Wakristo wanadhani maneno ya Yesu katika Mathayo 28:19
ni mepesi sana. Ukweli ni magumu sana kwani yamejumuisha neno gumu sana
la Roho Mtakatifu.
Rejea makala yangu ambayo bado kumaliziwa "Tafsiri sahihi ya Roho Mtakatifu"
(katika ANNUUR Na. (60).
Nikisema nitafsiri maneno hayo kiutaratibu ili kujua Yesu alimaanisha
nini, nitajaza si chini ya kurasa nne za gazeti. Hebu fikiria, neno moja
tu la Roho Mtakatifu kwa ufupi imeshindikana kumalizika katika kurasa moja,
sasa tukichanganya na maneno ubatizo, jina, baba na mwana itakuwaje?
Kwa ufupi sana Yesu aliposema kubatiza katika Mathayo 28:19 alimaanisha
kuwatoa wapagani katika hali ya kutomjua Mwenyezi Mungu na Mitume wake,
na kuwafanya (kuwabatiza) wawajue Mwenyezi Mungu, Mtume Yesu (as) na Mtume
atakayekuja baada ya Yesu (Roho Mtakatifu).
Kitendo cha kutosa majini ni uthibitisho (shahada) kuwa mtu ameshamwamini
Mwenyezi Mungu na Mtume anayehusika (aliyepo). Hivi sasa ubatizo (shahada)
kwa kutosa majini umeshafutwa kama alivyotabiri Mtume Yohana (as) ingawa
alidhani Yesu ndiye Mtume ambaye hatatumia ubatizo huo. "Akahubiri akisema,
yuaja nyuma yangu aliye na nguvu kuliko mimi ambaye mimi sistahili kuinama
na kuilegeza gidamu ya viatu vyake. Mimi niliwabatiza kwa maji, bali yeye
atawabatiza kwa Roho Mtakatifu", yaani watafanywa wamwamini Mwenyezi Mungu
na Mtume anayehusika kwa mafundisho matakatifu (Tazama ANNUUR Na. 60 Uk.
14 tafsiri Na (V) ya Roho Mtakatifu).
Sisi Waislamu tunabatizwa na kubatiza kwa Roho Mtakatifu kama alivyotabiri
Mtume Yesu (as) "Yesu akamwambia, mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu
Baba katika mlima huu (Gerizim) wala kule Yerusalem. Ninyi mnaabudu msichokijua,
sisi (Mitume) tunaabudu tukijuacho, kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.
Lakini saa inakuja nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba
katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu hao wamwabudu. Mungu
ni Roho, nao wamwabuduo Yeye imewapasa kumwabudu katika Roho na Kweli"
(Yohana 4:21-24.
Bwana Batendi anaendelea: "Au wakati Yesu alipotabiri kuwa wafuasi wake
watafukuzwa kwenye Misikiti (masinagogi) Yoh. 16:1-2, je, utabiri huo ulitimia
vipi? Ni kina nani waliobaki Misikitini?
Maneno haya yananitia mashaka juu ya elimu yake ya darasani. Hivi hajui
waliosema "sinagogi ni Msikiti wa Wayahudi" (Biblia Uk. 1229) ni wafasiri
wa Kiswahili wa Biblia wakizingatia kuwa Msikiti ni jengo (sehemu) la ibada.
Hivyo Kanisa nalo ni Msikiti wa Wakristo.
Hata baa ni "Msikiti" au "Kanisa" la walevi na Casino au danguro ni
hivyo hivyo wakimwabudu Mungu wao Shetani. Tazama 2 Wakorintho 4:4 na Ufunuo
3:9.
Mimi siwezi kulumbana na watu aina ya akina Batendi kwani siwezi kuelewana
nao. Ndio maana nawataka Wanatheologia wapinge makala zangu kama wana ubavu.
(Taz. ANNUUR Na. 145 Uk. 10) akina Batendi siwezi kuwa reffer kwenye vitabu
vinavyotumika katika vyuo vya theologia kwani hawavijui. Sasa tutaelewana
vipi!
Hata makala hii lengo lake sio kumjibu Bwana Batendi, bali nimetoa mfano
tu wa upuuzi unaofanyika. Imekuwa bahati mbaya sana kura imemwangukia Bwana
Batendi. Ningeweza kumtolea mfano hata Mwinjilisti Kusupa. Tena huyu Mwinjilisti
amenichoma sana kwa mahubiri yake aliyoyaingiza katika makala yake iliyo
katika ANNUUR Na. 162 Uk. 11.
Maneno yaliyo mwanzoni kabisa kifungu (b) yameniuma sana. Imekuwa kama
ameniambia mimi peke yangu. Hata hivyo imenibidi nijikaze sana nisimjibu
kwa sababu kwanza hatanielewa kwa kuwa ndo akina Batendi wenyewe, pili
atanichelewesha kwenda kupalilia mihogo yangu.
Hivyo kwa kuchelea kukumbwa na njaa, imenibidi niendelee kumvumilia.
Bwana Kusupa anapenyeza mahubiri yake katika gazeti la Kiislamu (ANNUUR)
kwa kutumia filosofia ya hali ya juu sana ambayo kwa mtu mwenye elimu ndogo
hawezi kugundua lengo lake.
Mwisho nawashauri Wanatheologia waache kudanganya watu. Wachukue mfano
mzuri wa Mchungaji A.T. Manoni. Tazama AN-NUUR Na. 144 Uk. 11 na Na. 158
Uk. 11 makala hizo ni sahihi kabisa. Kwa msimamo huo kama hajawa Muislamu,
huo ni mwanzo nzuri wa kuwa Muislamu.
Hata mimi nilianza hivyo hivyo kuyakubali mafundisho ya Kiislamu, kisha
baada ya miaka mitatu nilisilimu rasmi mwaka 1989 nikiwa na umri wa miaka
27.
Aidha nawashauri Wakristo wengine wasikubali kuburuzwa. Wazingatie maneno
haya Matakatifu "Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia
sana aendavyo" (Mithali 14:15).
|