AN-NUUR
Na.157 Rabi' Awal 1419, Julai 10 - 16, 1998
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Elimu ya Dini ya Kiislamu kwa Shule za Sekondari 
Somo: Tawhiid Form IV

Kuamini Qadar ya Mwenyezi Mungu (s.w.) 

Tatizo la Qudra 

Tangu zama na zama hadi hivi leo binadamu amekuwa akikabiliwa na swali gumu sana nalo ni hili: Je, sisi kama binadamu tunayo hiari ya uchaguzi katika maisha yetu (free will) au tunafuata tu njia ambayo ilikwishapangwa hata kabla ya kuzaliwa kwetu? Ugumu wa swali hili unatokana na kitendawili kifuatacho: 

(a) Kama tunayo mamlaka na uwezo kamili juu ya mwendo mzima wa maisha yetu Mwenyezi Mungu anayo nafasi gani? Tunaamini kuwa yeye peke yake ndiye mwenye mamlaka na uwezo usio na kikomo juu ya mambo yote na anayajua yaliyopita, yaliyopo sasa na yatakayotokea baadaye, vipi tena awe hana mamlaka juu ya mwendo wa maisha yetu? 

(b) Kama mwenendo mzima wa maisha yetu umekwishapangwa na Mwenyezi Mungu ambaye ni muweza wa kila kitu, kabla hata hatujazaliwa, kwa nini basi tuhisabiwe? Ikiwa Mwenyezi Mungu anauendesha ulimwengu huu kwa hikima na haki, kwa nini awahisabu watu kwa mambo ambayo tangu hapo Yeye ndiye aliyeyapanga? 

Mitazamo ya Wanafalsafa juu ya Qadar 

Wanafalsafa waliojaribu kukitegua kitendawili cha Qudra ni wengi sana na wanahitlafiana katika vipengele vingi. Hata hivyo kimsingi hoja za wanafalasafa hao zimegawanyika katika makundi makuu mawili. Kundi la kwanza linasema kuwa binadamu anayo mamlaka kamili juu ya mwenendo wote wa maisha yake na kwamba ingawa Mwenyezi Mungu anajua kila kitu lakini anajua tu baada ya tukio kutokea na siyo kabla. Wengine wanasema Mungu hayupo na hivyo binadamu ni mdhibiti wa kila kitu. Kundi la pili linasema Mwenyezi Mungu ana mamlaka kamili juu ya maisha yetu na halitokei jambo ila limeidhinishwa naye. Jitihada zote anazozifanya binadamu ni za kutupa nguvu bure kwani kila kinachotokea binadamu hana hiari yoyote. Wengine wanasema mwenendo mzima wa maisha ya kila binadamu umekwishapangwa lakini binadamu anaweza kujua kila alichopangiwa kama atajua namna ya kusoma mwenendo wa nyota yake au kitanga chake (n.k) lakini hataweza kubadili hata akijua kabla na wengine wanasema anaweza kubadili nuksi kuwa bahati akitoa kafara fulani n.k. 

Maana ya neno Qudra 

Kwa bahati mbaya mara nyingi hutokea utatanishi mkubwa sana juu ya maana ya Kudra hasa kwa watu wanaotegemea tafsiri ya Kiingereza ya neno hilo. Katika lugha hiyo Kudra hutafsiriwa kama "pre-destination" au "predetermination". Kitaalamu si makosa kuitafsiri Kudra kuwa ni "predestination". Kwa upande mmoja tafsiri hiyo ni sahihi. Lakini tatizo la tafsiri hiyo ni kuwa neno "predestination" katika lugha ya Kiingereza limebeba pia dhana ya kukata tamaa na moyo wa kuyandaa mambo yaende yendavyo (fatalism). Na hilo limewapelekea baadhi ya wanazuoni wa Kimagharibi wadai kuwa Uislamu unawafundisha wafuasi wake wawe na tabia hiyo ya kukata tamaa. 
 
 

Fiqh Form IV

Ndoa ya Kiislamu 

Maana ya Ndoa 

Ndoa ni mkataba wa kuishi pamoja kati ya mume na mke kwa kufuata utaratibu uliowekwa na jamii. Ndoa ya Kiislamu (Nikah) ni mkataba (Aqd) wa hiari kati ya mume na mke wa kuishi pamoja kwa wema na upendo kufuatana na masharti na taratibu zilizowekwa na sheria ya Kiislamu. 

Umuhimu wa Ndoa kwa Mtazamo wa Uislamu 

Katika Uislamu ndoa ni jambo lililokokotezwa sana kutokana na umuhimu wake katika kuijenga na kuiendeleza jamii. Ndoa kwa mtazamo wa Uislamu inatarajiwa: 

i) Kuihifadhi jamii na zinaa 

ii) Kuendeleza kizazi kwa utaratibu mzuri 

iii) Kujenga mapenzi, huruma na ushirikiano katika familia 

iv) Kukuza uhusiano na udugu katika jamii 

v) Kukilea kizazi katika maadili 

vi) Kumuendeleza mwanaadamu kiuchumi. 

(i) Kuhifadhi jamii na Zinaa 

Matamanio ya jimai ni katika maumbile na hayaepukiki.Wanyama pia wameumbwa na matamanio haya lakini yanatofautiana sana na yale yaliyopandikizwa kwa mwanaadamu. Matamanio ya jimai kwa wanyama yanakuja juu wakati maalum, wakati ule tu wanapokuwa tayari kupandikiza mbegu ya uzazi. Matamanio ya jimai kwa wanaadamu wa kawaida yako pale siku zote, mradi tu vipatikane vishawishi. Kwa hali hii, endapo mwanaadamu ataachiwa huru atosheleze matamanio yake ya jimai apendavyo pasina kuwekewa mipaka, kwa vyovyote patatokea madhara makubwa kwake binafsi na kwa jamii nzima. Hivyo, Mwenyezi Mungu (s.w.) aliyemuumba mwanaadamu kwa lengo na anayelifahamu vyema umbile la mwanaadamu na matashi yake kuliko yoyote yule, amemuwekea utaratibu madhubuti wa kukidhi haja zake za kimaumbile pasina kuleta kero kwa yeyote katika jamii. Mwenyezi Mungu (s.w.) ameharamisha jimai nje ya ndoa ili kuikinga jamii ya mwanaadamu na madhara makubwa ya zinaa ambayo huidunisha na kuivuruga kiasi kikubwa. Mwenyezi Mungu (s.w.) amehalalisha ndoa na kuitilia mkazo kwa wale wenye uwezo kama tunavyojifunza katika aya zifuatazo: 

"... Na mmehalalishiwa (kuoa wanawake) mighairi ya hawa. Muwatafute kwa mali zenu, kwa kuwaoa bila ya kufanya zinaa..." (4:24). 

"...Na (mmehalalishiwa kuwaoa) wanawake wema wa Kiislamu na wanawake wema katika wale waliopewa kitabu kabla yenu. (Ni halali kuwaoa) mtakapowapa mahari yao mkafanya nao ndoa bila ya kufanya uzinzi wala kuwaweka vimada..." (5:5). 

Aya hizi zinatubainishia kuwa ndoa ni ngao ya kujiingiza na kitendo kichafu cha zinaa. Pia Mtume (s.a.w.) amesisitiza ndoa kwa lengo hili hili la kujikinga na zinaa kama tunavyojifunza katika hadithi zifuatazo: 

Abdullah bin Mas’ud (r.a.) ameeleza kuwa Mtume (s.a.w.) amesema: "Enyi kongamano la vijana! Na aoe yule aliye na uwezo miongoni mwenu, hakika kuoa kunainamisha macho (ya matamanio) na kunahifadhi tupu (humzuia mtu na uzinzi). Na asiyeweza kuoa na afunge; hakika funga hukata matamanio" (Bukhari na Muslim). 

Pia Mtume (s.a.w.) amesema: 

Mmoja wenu atakapomuona mwanamke kisha akamtamani, hana budi kumuendea mkewe kwani ana kile kile alicho nacho huyo mwanamke aliyemtamani. (At-Tirmidh). 

Hadithi hizi zimesisitiza ndoa na kuonyesha umuhimu wake katika kuikinga jamii na zinaa. Uislamu kwa kusisitiza ndoa, umefunga njia zote zitakazo wapelekea wanaume na wanawake kutosheleza matamanio ya jimai nje ya ndoa. Uislamu umekataza uzinifu wa kila aina na umesisitiza ndoa ili kuwawezesha wanaume na wanawake baleghe, kukidhi matashi ya kimaumbile na wakati huo huo wawe na upendo na ushirikiano wa kudumu ili waweze kuwalea watoto watakaopatikana. 

(ii) Kuendeleza kizazi cha Mwanaadamu kwa utaratibu mzuri 

Lengo la ndoa haliishii kwenye kufurahia jimai tu bali kitendo hicho kinakusudiwa kiwe ndio sababu ya kupatikana watoto watakao endelezaa kizazi cha mwanaadamu. Lengo hili la ndoa linabainishwa wazi katika aya ifuatayo: 

“... Wala msiwaue watoto wenu kwa kuhofia umaskini.  Sisi tunakupeni riziki nyingi na wao pia...”   (6:151).
Kuchagua mchumba
 Ndoa ya Kiislamu inataratibu zake kuanzia kwenye kuchagua mchumba mpaka kukamilisha ndoa.  Yakuzingatia katika kuchagua mchumba ni:
i) Dini
ii) Tabia njema
iii) Umaharimu
iv) Sifa nyinginezo
(i) Dini

Jambo la kwanza atakalo lizingatia Muislamu katika kutafuta mchumba ni dini.  Waislamu wanaume wameruhusiwa kuwaoa wanawake wema wa Kiislamu na wanawake wema katika wale waliopewa Kitabu kabla ya Qur’an. Ruhusa hii tunaipata katika aya ifuatayo:

“...Na (mmehalalishiwa kuwaoa) wanawake wema wa Kiislamu na wanawake wema katika wale waliopewa kitabu kabla yenu, mtakapo wapa mahari yao na kufunga nao ndoa, bila ya kufanya uzinifu au kuwaweka kinyumba...” (5:5).

Katika aya hii tunaona ruhusa iliyotolewa na Mwenyezi Mungu (s.w.) kuwaoa wanawake wema wa Kiislamu.  Msisitizo wa kuoa wanawake walio wema tutauona katika kipengele cha (ii).  Ama kuhusu ruhusa ya kuwaoa wanawake wema miongoni mwa wanawake wa Ahlal-Kitaabi, kuna mawazo tofauti tofauti kutoka kwa wanavyuoni.

Kulingana na Sheikh Abdallah Saleh Alfarsy katika sherehe ya aya hii (5:5) uk. 146, ameeleza kuwa Mkristo anayeruhusiwa kuolewa na Muislamu ni yule tu ambaye ukoo wake umeingia katika dini hiyo kabla ya Uislamu haujaja.  Amezidi kusisitiza Sheikh “Ama hawa wanaoitwa Misheni wanaoingia katika Ukristo sasa si halali kuwaoa.  Ni haram wala ndoa haisihi”.

Kulingana na maoni ya Ibn Abbas (r.a.), Muislamu anaweza kumuoa mwanamke wa Ahlal-Kitaabi aliye katika himaya ya Dola ya Kiislamu tu, na haruhusiwi kumuoa mwanamke wa Ahlal-Kitaabi ambaye yuko katika dola ambazo ni maadui wa Dola ya Kiislamu au yuko katika dola za Kikafiri.  Tofauti na maoni haya ya Ibn Abbas, Said bin Masayyab na Hassan Basri* wanasema kuwa ruhusa hii ya kuwaoa wanawake wema wa Ahlal-Kitaabi imetolewa kwa ujumla na hapana haja ya kufanya ubaguzi wowote kati ya Ah-lal-Kitaab.

Ieleweke kuwa kuwaoa Ahlal-Kitaabi si amri bali ni ruhusa kutoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.) kama ruhusa nyingine zilizotolewa katika Qur’an.  Kuitumia ruhusa hii pasina haja na pasina kuzingatia malezi ya watoto katika misingi ya Uislamu ni hatari kubwa.  Ikitokea mtu anaishi katika nchi ya Ahlal-Kitaabi na hana namna ya kumpata mwanamke mwema wa Kiislamu wa kumuoa,  itakuwa kwake vyema kumuoa mwanamke mwema miongoni mwa hao Ahlal-Kitaabi badala ya kufanya uzinifu au kukaa na mwanamke bila ndoa.  Ama pale ambapo kuna mabinti wema wa Kiislamu, kuna haja gani ya kumuoa binti wa Kikristo?  Jambo la msingi la kusisitiza hapa ni kwamba, aliyetoa ruhusa hii ni Mwenyezi Mungu (s.w.), Mjuzi Mweye Hekima, Hivyo, kwa vyovyote vile, kuna hekima kubwa katika ruhusa hii.  Tusije tukajiingiza katika makosa kwa kuchukia jambo aliloliruhusu Mwenyezi Mungu (s.w.).

Ni haramu kwa wanawake wa Kiislamu kuolewa na Wanaume Wakristo au Mayahudi.  Hivyo kwa mtazamo wa Kiislamu hapana ndoa kati ya mwanamume Mkristo au Myahudi na mwanamke Muislamu.  Mtu atakayemwozesha binti yake kwa Mkristo, ajue wazi kuwa amemruhusu zinaa.  Vile vile kwa Waislamu ni haramu kushiriki katika sherehe za ndoa za namna hiyo kama ilivyo haramu kushiriki katika sherehe zote za kidini za Makafiri, Washirikina na Ahalal-Kitaabi.  Kusherehekea pamoja nao, moja kwa moja, ni kuwaunga mkono katika hayo wanayosherehekea kinyume na Mwenyezi Mungu (s.w.).

Waislamu wanaume na wanawake wameharamishiwa kuoana na makafiri na washirikina kama inavyobainika katika aya ifuatayo:
Wala msiwaoe wanawake makafiri mpaka waaamini. na mjakazi mwenye kuamini ni bora kuliko muungwana kafiri, hata kama amekupendezeni.  Wala msiwaoze waaume makafiri (waawake wa Kiislamu) mpaka waamini.  na mtumwa mweye kuamini ni bora kuliko muungwana kafiri, hata akikupendezeni.  Hao makafiri wanaitia kweye moto.  Mweyezi Mugu wanaitia kwenye Pepo na Samahani kwa amri yake. (2:221).
 

Juu 
 

YALIYOMO
 

TAHARIRI 

Maoni yetu: Prof. Juma Kapuya, vipi Muislamu usijue agenda za Waislamu? 

Hatimaye Mzee Katambo, Chata waachiwa
Na Mwandishi wetu

Polisi Newala wajenga Msikiti 

Sheikh Bafadhil aitaka Bakwata iwe mtetezi wa Waislamu
Na mwandishi wetu

Makala: Uinjilisti wa Mbuni haufai
Na Rajabu Mbambwa, Kigoma

Mussa Katambo: Mzee aliyewekwa rumande kwa kuandaa mihadhara

Ukweli usiachwe 

Makala: Elimu ya ngono yapenyezwa tena Zanzibar 
Na Saidi Mzee 

Arusha wasema: Hongera Mhe. KK kwa kuwa mfano mwema 
Na Hussein M.,  Arusha 

Wanawake Songea kuandaa maonesho 
Na. Jumah Mbwana, Songea 

Kesi ya mgogoro wa Ardhi
Na. Mustafa Adam 

AN-NUUR marufuku gerezani? 
Na Mwandishi Wetu 

Waislamu Karagwe wadai kusalishwa na imamu asiyejua kutawadha 
Na. Abu Abdallah 

Ofisi mpya za Rabita 
Na Mwandishi Wetu

Barua za wasomaji

Habari za Madrasa

Masomo

 

 
 Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu:
Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtanzania.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita