|
|
Japo ziara hiyo ilikuwa ni ya kidini, watu wa dini zote walijitokeza kumshangilia kila alipopita. Hoi hoi zilianzia uwanja wa ndege wa mjini Mwanza ambapo wasafiri walijisahau na kuungana na wasindikizaji na kuanza kumshangilia Rais huyo mstaafu kwa nguvu. Wasafiri hao ambao walikuwa wakisubiri ndege ya ATC kuelekea Dar es Salaam bila kujali kupoteza au kuibiwa mizigo yao walijikuta wakijumuika na wafanyakazi wa Uwanja huo katika fujo la shangilio la aina yake lililomkaribisha Alhaj Mwinyi mara baada ya kushuka kwenye ndege iliyomleta kutoka Dar es Salaam. Katika kila njia alikopita watu walijitokeza kwa wingi kumshangilia huku wengine wakitoa sauti ya juu kukariri hali ilivyokuwa nyuma wakati anachukua uongozi na neema aliyowaachia wakati anaondoka. Akiwa Nyakato, umati mkubwa wa aina yake ulijitokeza bila kuhamasishwa na kuanza kupaza sauti kumshukuru kwa yote mema aliyowatendea wananchi. Ratiba ya Alhaj Ali Hassan Mwinyi mjini Mwanza ilianza kwa kuhudhuria mashindano ya kusoma Qur’an katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa ambayo yalianza saa 4:20 asubuhi hadi saa 8:50. Katika mashindano hayo mtoto Hudhaifa bin Saleh Hazaa mwenye umri wa miaka tisa alishinda. Mtoto Hudhaifa anasoma katika kituo cha kuhifadhia Qur’an cha Ibn - Masoud kilichopo Bwiru, amehifadhi juzuu ishirini. Vyuo vingine vilivyoshiriki ni Nyakato Islamiya, Taqwa Madrasa, Thaqaafa Muslim School, Khalqa-Nyakato, Habibu Swaleh - Nyakato, Madrasa Fallah - Kirumba na Madrasa Khayria - Nyakato. Madrasa zilipangwa katika makundi kufuatana na washindani walivyohifadhi. Kundi A - Juzuu moja, kundi B juzuu mbili, kundi C juzuu tatu, kundi D juzuu nne. Kundi E juzuu tano, kundi F juzuu sita, kundi G juzuu nane. Mshindi wa jumla katika madrasa walikuwa Madrasa ya Habib Swaleh chini ya Ustadh Kibira, walipewa kikombe moja kwa moja kutokana na kushinda mfululizo mara tatu. Mgeni rasmi Rais Mstaafu Alhaj Mwinyi alitumia nafasi hiyo kwa kupongeza ushirikiano aliouona tangu afike Mwanza na alihimiza ushirikiano miongoni mwa Waislamu ili kujiletea maendeleo. Alisisitiza kuepukana na dharau miongoni mwa Waislamu, taasisi na vikundi mbalimbali vya harakati za Kiislamu, alisema kila taasisi iendeshe shughuli zake kama ilivyoamua bila ya kuingiliwa madamu lengo ni kuupeleka Uislamu mbele. Alisema ni ruhusa kila madhehebu kuendesha ibada kwa mujibu wa mapokezi yao maadam hawavunji nguzo za sala. Siku hiyo baada ya mashindano hayo alihudhuria chakula cha mchana nyumbani kwa Mwenyekiti wa madhehebu ya Ibaadh Sheikh Nassoro Ally Farai. Siku iliyofuatia aliweka mawe ya msingi katika chuo cha Habib Swaleh kilichopo Nyakato, Nyegezi na Mkoani wakati mchana wake alihudhuria karamu ya chakula nyumbani kwa Bw. Mustapha Hassan Manengero nyuma ya mtaa wa Uhuru. Siku hiyo hiyo jioni alitembelea
kituo cha yatima Ilemela; kuweka jiwe la msingi la madrasa Taqwa na kuhudhuria
chakula cha usiku kilichoandaliwa maalum shuleni hapo kwa ajili ya kutunisha
mfuko wa ujenzi wa shule nyingine ya Kiislamu chini ya shule hiyo hiyo
ya Taqwa sekondari Mwanza.
|
YALIYOMO
Tahariri Hakuna Idd kwa wanafunzi Waislamu mwaka huu Baada ya wanafunzi Wakristo kusherehekea Krismasi: Wanafunzi Waislamu kuikosa Id el Fitr Hoi hoi zatawala ziara ya Mwinyi Mwanza Waislamu Tunduma waswali ndani ya kilabu cha ulanzi MARADHI YA KISAIKOLOJIA: FROTTEURISM Barabara za Tabora zimepitwa na wakati Jicho la
Uzalendo: Nihiari yetu kuendelea kujidanganya!
Kuanza na kwisha mwezi wa Ramadhani Taarifa ya Kamati juu ya yaliyotokea Mwembechai Maazimio ya kongamano la wanawake wa Kiislamu Waislamu kijijini Kidunda Moro wahitaji mwalimu Waislamu Mtwara wadai jengo la Wakfu kwa CCM Wakati Makanisa yakimeremeta: Msikiti wageuka gofu Sanya Juu Sheikh Khalifa Suleiman afariki dunia Sheikh wa wilaya ya Lushoto afariki Ijue Madrasat Riyaadhwa ya mjini Dodoma Mwinyi apongeza juhudi za kulea yatima Mwanza Tuhuma za kupindua uongozi wa Bakwata: Sheikh Hamim Boza akanusha kuhusika Kuongezeka kwa ajali za barabarani Njia ya
uzimani ni nyembamba, waionao ni wachache - 4
Saggaf awataka watoto wahifadhi Qur'an Waislamu watakiwa kujitolea kupigania dini yao Kesi nyingine Mwembechai yaahirishwa Sayansi
na Teknolojia
Chakula
na lishe
|