|
|
| Serikali
izungumze na wananchi–Mzee Gonga
MTAALAMU maarufu wa lugha ya Kiswahili nchini, Mzee Shaaban Gonga amesema kwamba haoni ni kwanini viongozi wa serikali wakwepe kwenda kuongea na wananchi wa Nzasa kabla na baada ya kuchomewa nyumba zao wakati wale ni wananchi. Kauli hiyo ya Mzee Gonga imekuja kufuatia kilio cha wananchi wa Nzasa kwamba wangependa kuonana na Mh. Rais ili kumweleza kilio chao na azione hali zao. Mzee Shaaban Gonga akiongea na mwandishi wa habari hizi hivi karibuni alisisitiza kwamba haki hii ya wananchi kusikilizwa ni ya msingi sana kiasi kwamba hata wakati wa ukoloni wenyeji walipewa haki ya kutoa maoni yao na ndio maana walimpeleka Mwalimu Nyerere Umoja wa Mataifa ili kutoa maoni yao. Akisisitiza nukta yake hiyo, alinukuu kutoka kitabu alichokuwa amekishikilia ‘TANU katika UNO’ sehemu isemayo kwamba "wenyeji wanayo haki kutoa maoni yao kwa wajumbe hao juu ya jambo lolote na pia wanayo haki kuliandikia Baraza la Udhamini kulieleza shida zao au jambo lolote jingine". (TANU katika UNO Uk. 2 Kf. 3). Ni kutokana na ukweli huo, Mzee Gonga alihoji wakati ule wananchi walipata haki kuongea na Baraza huku tunatawaliwa na Mwingereza, vipi leo ishindikane serikali kuongea na wananchi wa Nzasa. Kuhusu mgogoro wa Nzasa – Kazimzumbwi kwa ujumla Mzee Shaaban Gonga alisema kwamba kitovu cha yote ni suala la haki ya mwananchi katika ardhi. Alisema suala la ardhi sio la mzaha na ndio lililokuwa limetawala hisia za watu katika kudai uhuru. Na vile vile ndio maana TANU katika UNO ilitamka wazi kwamba: " Hatutaki ardhi yoyote ambayo haijakodishwa kwa wageni ikodishwe tena. Na tumefurahi kusikia kuwa Gavana ametamka hadharani kuwa hakuna ardhi tena ya kuwapa wageni mbalimbali", alinukuu mzee Shaaban Gonga katika kitabu cha TANU katika UNO. Alisema Mwalimu Nyerere alipotumwa UNO alisisitiza kwamba yawezekana hatuna elimu, lakini tuna ardhi, hivyo anashangaa leo mwananchi anachezewa katika suala nyeti la ardhi. Alisema pengine itabidi wazee wazungumze na mzee mwenzao Mwalimu Nyerere kabla hawajafa maana miaka 37 baada ya uhuru bado mwananchi hana haki juu ya ardhi yake alikozaliwa na kuishi. Mzee Shaaban Gonga ambaye wakati TANU inaanzishwa ndio walikuwa vijana wakitumwa sehemu mbalimbali katika harakati za kudai uhuru, amesema kwamba mgogoro wa ardhi Nzasa una historia ndefu. Wakati wa ukoloni, kuna Giriki alitaka kuchukua ardhi yote yenye rutuba inayojumuisha vijiji vya Kazimzumbwi, Kisanga, Mvuti, Dondwe, Kisimba, Bupu na Maruwi. Hata hivyo akasema Mzee Muhunzi kwa niaba ya wananchi alishitaki serikali ya wilaya na Giriki akazuiwa. Hoja kubwa ilikuwa wananchi waende wapi, alieleza na kuhoji. "leo vipi huyo Mtimkavu kudai haki ya wananchi wa Nzasa iwe nongwa. Hii ni mazingira au yupo Giriki mwingine?" Kwamba Nzasa ni wahamiaji au wavamizi, Mzee Gonga alisema kwamba hilo haliwezekani. Akasema kwamba wakati Dar es Salaam Boma lipo Avalon ya leo, Boma la Kisarawe lilikuwa Chang’ombe eneo la Kioo Ltd. Mji ulivyopanuka likahamiashiwa Nzasa kwa vile kulikuwa na watu. Hata hivyo, akasema kwamba Boma lilikaa kwa muda hapo likahamia Kilimani Kisarawe lilipo leo. Kuambiwa wananchi wa Nzasa ni wavamizi inashangaza alisema. Katika suala zima la haki ya wananchi katika ardhi, Mzee Shaaban Gonga alisema kwamba mwananchi hafukuzwi kwa kuonyeshwa jiwe au hati. Unamwonyesha jiwe upate kumuhamisha aende wapi, alihoji. Kama ni hati za miaka thelathini au tisini na tisa hizo stahiki yao wageni. Sio mwananchi. Yeye kwake. Huwezi ukamwondoa katika ardhi, na nchi yake bado akawa mwananchi. Alisema makabila yote yalikuwa na utaratibu na mpangilio wa ardhi. Lilikuwepo
eneo la kujenga mji, eneo la kilimo na eneo la jamii. Kwamba pale watakwenda
kuwinda, kuokota kuni, kutambika, kuchimba dawa n.k. Katika mazingira hayo
ya kiasili kila Gavana alipotaka kuingilia wazee walikusanyika na kuhoji
tukalime wapi, tukaokote kuni wapi, wake zetu kaniki watapata wapi. Maswali
hayo yalipowashinda Giriki alinyimwa eneo, alisema na kuhoji kwa masikitiko,
"leo Nzasa inachomwa moto wapo wapi kina Mzee Muhunzi".
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Wasomi watetea haki ya wananchi kumiliki ardhi Serikali izungumze na wananchi–Mzee Gonga Akina mama watakiwa kushikamana na dini yao Maoni
Dondoo
za Saikolojia: Hoja kengeza
Makala ya mtangazaji
Makala
Tanzania
tuna sera gani kuhusu kanda
Mdahalo
kati ya Waislamu na Wakristo- 2
Teknologia
Makala na habari
Mwinyimkuu
kufanya sensa ya waumini Magomeni
Wazazi
Mwanza wahimizwa kuwashonea watoto wao Hijab
Tuwaige
Wangazija, 'tutafanikiwa'
Serikali
imeweka rekodi ya kutisha – Sheikh Salim
Muhadhara
waunguruma Geita
Fuateni
Sharia ya Allah - Sheikh
Wanawake wa Kiislamu Mburahati wahimizwa kutafuta elimu Mafunzo
ya Qur'an
Chakula na lishe
|