|
|
Ni kawaida iliyozoeleka nyumba ikiwa imo katika eneo lisiloruhusiwa; hubomolewa, tena wakati mwingine baada ya kutolewa fidia. Haikuwa hivyo kwa nyumba ya Bw. Mohamed Hassan na mkewe Tausi Rashid, yao ilichomwa moto. Haikuwa hivyo kwa Bw. Omar Sadala (67) yake iliteketezwa kwa moto na akiba yake yote ya chakula kuangamizwa. Hali ilikuwa tofauti kwa Bw. Juma Mohamed na mkewe Zaina Athumani walichoweza kunusuru ni roho zao na kitanda chao cha kamba, wakiishia kuanza makazi mapya chini ya mti bila chakula baada ya kila chao hata makopa ya akiba kuteketezwa kwa moto! Waliovamia fukwe za bahari na viwanja vya michezo na kujenga mahekalu hatunayo majina lakini ni wazi hayawezi kuwakuta yaliyomkuta Mzee Juma Abdallah ambaye aliambulia kuokoa gogo alilokuwa akitumia kama kiti baada ya nyumba yake kuchomwa moto. Wala hawawezi kupatwa na masaibu yaliyomkuta Bibi Khadija Rashid (65) ambaye hata kitanda na kinu alichofanikiwa kuokoa na kuficha porini havikusalimika baada ya pori lenyewe kuchomwa moto! Ni wazi vile vile kwamba watoto wao hawatakosa kwenda shule kama ambavyo watoto wa Halima Mkongwa na Habiba Mwalimu wameshindwa kwenda baada ya sare zao za shule kuunguzwa moto. Pamoja na amri ya Serikali ya kuwataka wananchi wa kijiji cha Nzasa wahame katika eneo linalodaiwa la hifadhi ya msitu wa Kazimzumbwi, hatukutarajia zoezi la kuwahamisha wananchi hao lichukue sura ya kutojali wala kuthamini uhai na mali za wananchi. Wapo watoto; waja wazito, vilema, wagonjwa na vikongwe. Wengine tunaambiwa wanajifungulia kwenye matuta baada ya nyumba za kuchomwa. Angalau vingetembezwa virungu kuwaswaga watu ndani ya karandinga kuwapeleka makazi mapya. Maana hata kiwete ukimburura unamsaidia kufika haraka. Lakini moto! Hawa ni wananchi ambao walitekeleza wajibu wao wa kupiga kura kuiweka serikali iliyopo madarakani, michango ya mwenge wanatoa, huhudhuria mikutano ya hadhara huku wakiungua jua bila kudai posho ya kikao; huwapigia makofi viongozi wao hata bila ya kuelewa wanachosema, hujitibu wenyewe na kuwasomesha watoto wao wenyewe wala hawajauliza kodi na michango wanayotoa inafanyia kazi gani na pengine hutoa hata majina ya wala rushwa. Wanapounguziwa moto nyumba zao nia na lengo ni kuwahamisha au kuwaangamiza! Hata kama ni jambazi lililoua, achilia mbali kuvamia msitu; basi zipo taratibu za kisheria za kuliadhibu. Si kulichoma moto lenyewe au nyumba yake. Na hata kama ni katika vita, basi haiwi mmeteka kijiji katika nchi adui halafu mnachoma nyumba za watu mliowakuta ambao si askari walioshika silaha; sikwambii raia wapiga kura wako! Baadhi ya taarifa zimefahamisha kwamba mgogoro huu ulifika hadi katika vyombo vya sheria, hukumu ikatolewa wasihamishwe. Lakini shinikizo lilipozidi hawa akina Rashid Hemed, Juma Chaubaya, Maryamu Juma wakadai wapewe japo fidia ili wakitoka hapo wajue wanakwenda wapi. Jibu likawa hampati kitu. Sasa Bw. Juma Chaubaya anasema atafia porini maana hana pa kwenda. Atapataje pa kwenda wakati hakuwa na raslimali zaidi ya shamba lake la muhogo, kitanda cha kamba, zaidi ni nguo aliyovaa. Hana senti benki wala ghala la mbaazi na muhogo. Muhogo, kibanda na kitanda vimegeuzwa jivu; aende wapi! Tatizo hapa si wananchi hao kuhama au kutokuhama, lakini hii hali ya inayoonekana ya kikatili. Vyovyote iwavyo, hawa ni wananchi. Haistahili kufanyiwa unyama wa kiwango hiki. Mzazi kumwambia mtoto wake ukiwapeleka mbuzi machungani nitakupa chakula; nguo kukupeleka shule na kukulea kwa ujumla; huwa kichekesho. Nini maana ya kuwa baba kama jukumu la kulea halipo. Mtoto umwambie ukifaulu hesabu nitakununulia baiskeli. Sio ukifaulu fizikia nitakulea. Wananchi walijitolea muhanga kuondoa utawala wa kikoloni kwa sababu ulikuwa wa kibabe, kibaguzi na kidhalimu. Walitamani utawala wa haki na sheria, na zaidi wenye kuwajali na kuthamini uhai wao na mali zao. Kama ilivyo kichekesho baba kuahidi kumlea mtoto kama zawadi; ilifikia mahali suala la "Utawala wa Haki na Sheria" kufanywa jukwaa la kuombea kura. Pamoja na hayo, wananchi walishukuru kwamba huenda yale
ya "Kilombero" na "operesheni vijiji" ikawa ndio mwisho, lakini tukio hili
linatuweka kwenye utata mkubwa. Ni mfumo gani hasa wa serikali yetu, maana
ipo mingi. Nani aliyeagiza kufanywa operesheni hii? Je, aliagizwa na Mh.
Rais; au je, Mh. Rais aliombwa ruhusa ? Na kimya hiki je, Mh. Rais hajapata
habari? Ameridhika!
|
YALIYOMO
TAHARIRI
Waislamu wasisitiza: Nyumba ya Waziri
Mkuu ni ya Waislamu
Kuchomwa nyumba za wananchi
Maoni Yetu:
Nguruwe marufuku Kinondoni – Tume
Watanzania waanzisha Baraza la Waislamu
Marekani
Wanawake Hai wamtaka Rais azungumzie
mauaji ya Mwembechai
‘Serikali haiwezi kuzuia rushwa’
Makala ya Kimataifa
Afghanistan washindi dhidi
ya uvamizi karne zote
MAKALA:
Tujikwamue na janga la utwaghuti
MAONI:
MAKALA:
Tufuate Uislamu kwa vitendo
na siyo kwa maneno -2
Tusihalalishe mauaji ya
raia kwa kisingizio cha ‘wananchi wenye hasira’
Historia ya sayansi na tiba
Msiwageuze watoto ombaomba
MAKALA YA JAMII:
Sensa ya majaribio: Wananchi watofautiana
na serikali
Uislamu ulivyoingia Zanzibar -3 Mwembechai wageuka Hame,
Bado walindwa na polisi
Waislamu Moro waendelea kusaidia
wagonjwa
Mjadala wa Katiba ya Shirikisho
kuzinduliwa Dar Jumapili
Walimu wa dini Tanga wapokea
Baiskeli
Mafundisho ya Quran
Chakula na Lishe
|