Wasomi Waislamu kutoka taasisi za elimu ya juu za Tanzania wamelaani
mauaji ya Waislamu yaliyofanywa na
jeshi la polisi katika maeneo ya Msikiti wa Mwembechai hapo Aprili
13, 1998.
Wasomi hao pia wameshangazwa na hatua za chama tawala (CCM) na Serikali
yake kuwapongeza wauaji. Vile
vile Waislamu hao waliisihi Serikali kuunda tume huru ya kuchunguza
mauaji na kuacha uonevu wa kuwanyima
dhamana watuhumiwa, ambao wengi wao ni wagonjwa, kwa visingizio ambapo
wamedai havina msingi
wowote.
Sambamba na hayo, wasomi hao walimpongeza Bwana Kitwana Kondo Mbunge
wa CCM jimbo la Kigamboni
kwa kuwajibika kwake kama Muislamu na pia kama Mtanzania, kuiambia
wazi Serikali juu ya chuki iliyonayo
dhidi ya Waislamu.
Wasomi hao waliyasema hayo katika sherehe za kuadhimisha mwaka mpya
wa Kiislamu, 1419 na kuwaaga
wanaomaliza masomo yao katika muhula huu wa masomo.
Sherehe hizo zilifanyika Mei 23, mwaka huu katika Chuo cha Maendeleo
ya Uongozi (IDM) cha mjini
Morogoro na kuhudhuriwa na wasomi Waislamu kutoka chuoni hapo, Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo
Kikuu cha Sokoine, Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Chuo cha Uhasibu
(DFA) cha Dar es Salaam na
Sekondari za Dar es Salaam na Morogoro
Katika sherehe hizo ziliichangwa shilingi 80,870/- kwa ajili ya kulipia
gharama za kuendesha kesi
zinazowakabili Waislamu kutokana na tukio la Mwembechai.